Mshambuliaji wa Kimataifa wa          Tanzania anayekipiga katika timu ya KRC Genk ya Ubelgiji, Mbwana          Samatta jana ameing'arisha Taifa Stars kwa kuifungia mabao          mawili na kuipa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Botswana.
        Mchezo huo wa kirafiki wa          Kimataifa ulio katika kalenda ya FIFA, umepigwa katika dimba la          Taifa Dar es Salaam na kushuhudiwa na maelfu ya watanzania          wakiongozwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo          Dkt. Harrison Mwakyembe alikuwa mgeni rasmi, akiambatana na          aliyekuwa waziri wa wizara hiyo, Nape Nnauye.
        Katika mchezo wa leo ambao          umejumuisha kikosi kipya kabisa cha Taifa Stars, chini ya kocha          mpya Salum Mayanga, kimeanza kwa kasi ya aina yake na kufanikiwa          kupata bao la mapema kabisa kunako dakika ya 2 mchezo kupitia          kwa nahodha Mbwana Samatta aliyeitendea haki pasi ya Mohamed          Hussein.
        Taifa Stars iliendelea kuonesha          kandanda safi, licha ya ubora na uimara wa Botswana, lakini          ikashindwa kutumia nafasi kadhaa ilizopata kupitia kwa Samatta,          Ajibu na Msuva.
        Kipindi cha pili kilianza kwa          Botswana kuongea nguvu na kufanya mashambulizi mengi ambayo hata          hivyo ukuta wa Taifa Stars uliokuwa ukiongozwa na Abdi Banda,          Erasto Nyoni, Mohamed Hussein na Shomary Kapombe uliweza kutulia          na kuhimili.
        Mabadiliko ya kuwatoa Shiza          Kichuya, Frank Domayo, Ibrahim Ajibu na Himid Mao na nafasi zao          kuchukuliwa na Farid Musa, Mzamiru Yasin, Salum Aboubakary na          Jonas Mkude, yaliweza kuzaa matunda ambapo katika dakika ya 77          Mwana Samatta akaifungia Taifa Stars bao la pili kwa mpira wa          adhabu alioupiga baada ya kuangushwa nje kidogo ya eneo la 18.
        Hadi mwisho wa mchezo, Tanzania          inaondoka na ushindi wa mabao 2-0, ushindi ambao una faida          katika viwango wa vya ubora ambavyo hutolewa naFIFA kila mwezi.
        
Comments
Post a Comment