Yanga Waandaliwa Mapokezi ya Kihistoria....!!!


Yanga Waandaliwa Mapokezi ya Kihistoria....!!!

Wawakilishi wa Tanzania katika michuano ya Klabu Bingwa Barani Afrika timu ya soka ya Yanga wanatarajia kurejea nchini mapema kesho wakitokea nchini Comoro ambako walikwenda kucheza mchezo wa awali dhidi ya wenyeji wao Ngaya.

Yanga ambayo itawasili majira ya saa tano asubuhi kwa saa za Afrika Mashariki wanataraji kupata mapokezi ya aina yake kutoka kwa maelfu ya wanachama na mashabiki wa soka hasa mashabiki wa klabu hiyo ambao watajazana katika Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere kuwasubiri mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Kuelekea mapokezi hayo makubwa tayari baadhi ya matawi ya wanachama wa klabu hiyo sehemu mbalimbali jijini Dar es Salaam wameshaanza vikao kwa ajili ya kuandaa mapokezi makubwa ya wawakilishi hao wa Tanzania.

Wakiongea na Eatv baadhi ya wanachama hao wamesema lengo la kuwapa mapokezi hayo makubwa na ya aina yake ni katika hali ya kuwapongeza wachezaji kwa kazi nzuri waliyofanya huko ugenini na kuibuka na ushindi mujarabu na pia kuwapa moyo wa uwajibikaji mzuri wakijua kuna mamia ya watu nyuma yao jambo ambalo litawahamasisha zaidi wachezaji kufanya vyema katika mchezo wa marudiano utakaopigwa siku ya Jumamosi Februari 17 mwaka huu katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Yanga SC wameanza vizuri mawindo yao ya ubingwa wa Afrika, baada ya kuwachapa wenyeji Ngaya Club de Mde mabao 5-1 jioni ya jana mjini Moroni, Comoro.


Comments