Tanzania Yaporomoka Kwa Nafasi 16 Viwango vya FIFA



Tanzania Yaporomoka Kwa Nafasi 16 Viwango vya FIFA

Tanzania imeporomoka kwa nafasi 16 katika viwango vya soka vya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) kwa mwezi Novemba

Kwa mujibu wa orodha mpya iliyotolewa leo (Novemba 24) na FIFA, Tanzania imeshuka kutoka nafasi ya 144 mwezi Oktoba hadi 160 mwezi huu kati ya mataifa 205 ambayo ni wanachama hai wa FIFA.

Kushuka huku kwa viwango kunatokana na kujikusanyia pointi 146 ikilinganishwa na pointi 212 ilizokuwa nazo mwezi Oktoba, ikiwa imecheza mchezo mmoja wa kirafiki dhidi ya Zimbabwe na kupoteza kwa kipigo cha mabao 3-0.

Kwa upande wake Zimbabwe, imepanda kwa nafasi 8 kutoka nafasi ya 110 hadi ya nafasi ya 102.

Kwa mataifa ya Afrika Mashariki Rwanda imepanda kwa nafasi sita hadi nafasi ya 101 wakati Kenya ikishuka kwa nafasi 4 hadi ya 89 na Uganda imeshuka kwa nafasi moja kutoka 72 hadi 73 ikiwa ndiye kinara wakati Burundi imepanda kwa nafasi 5 kutoka nafasi ya 138 hadi 133

Mataifa mengine katika ukanda wa CECAFA, Ethiopia imepanda kwa nafasi 11 hadi nafasi ya 115, huku Sudani ikipanda kwa nafasi 8, kutoka nafasi ya 148 hadi ya 140.

Afrika inaongozwa na Senegal nafasi ya 33 ikifuatiwa na Ivory Coast nafasi ya 34, Tunisia nafasi ya 35, Misri 36 na Algeria ni ya 38.

Katika 10 bora, Argentina imeendelea kushika nafasi ya Kwanza ikifuatiwa na Brazil, Ujerumani, Chile, Ubelgiji, Colombia, Ufaransa, Ureno, Uruguay na Hispania.


Comments