KOCHA ANCELOTTI ASEMA GUARDIOLA AMEMWACHIA KAZI NYEPESI MANCHESTER CITY




KOCHA ANCELOTTI ASEMA GUARDIOLA AMEMWACHIA KAZI NYEPESI MANCHESTER CITY
KOCHA wa Bayern Munich, Carlo Ancelotti amedai kuwa ameachiwa kazi nyepesi na aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Pep Guardiola ambaye amejiunga na klabu ya Manchester City.

Ancelotti amesema kuwa anaamini atafanikiwa katika klabu hiyo ya Bayern Munich kutokana na Guardiola kuiwekea njia ya mafanikio klabu hiyo.

Guardiola akiwa katika klabu hiyo ya Bayern alifanikiwa kutwaa mataji saba katika misimu mitatu ambayo aliitumikia ikiwa pamoja na kutwa taji la Bundesliga.

Ancelotti amedai kuwa anavutiwa na uezo wa wachezaji hao ambao umeachwa na kocha Guardiola.

"Ni kazi nyepesi sana kwa sasa katika klabu hii kwa kuwa nimewakuta wachezaji wakiwa katika ubora wa hali ya juu."

"Ninaamini ubora wa timu hii umeachwa na Guardiola, nimeikuta timu ikiwa katika ubora wa hali ya juu hivyo sina kazi kubwa ya kuifundisha."

"Misingi ambayo imeachwa na Guardiola ninaamini siwezi kuiacha au kuibadilisha kwa sasa kwa kuwa mizuri na itanipa mafanikio, japokuwa nina mipango yangu ambayo ninaweza kuiweka hapa," alisema Ancelotti.

Bayern Munich kwa sasa inashika nafasi ya kwanza katika msimu wa Ligi ikiwa na pointi 16 huku nafasi ya pili ikichukuliwa na Hertha Berlin ambayo ina pointi 13 baada ya timu hizo kucheza michezo sita.

"Ninajua kwamba timu yangu inafanya vizuri. Nimekuwa nikiiangalia timu hii kwa misimu mitatu iliyopita, hivyo kikubwa ni kuendelea na kasi hii kwa ajili ya kuipa mataji," aliongeza.


Kocha huyo mwenye umri wa miaka 57 aliwahi kuzifundisha klabu kubwa duniani kama vile AC Milan, Paris Saint-Germain, Real Madrid pamoja na Chelsea.


Comments