JUAN MATA AANZA MAZUNGUMZO YA KUSAINI MKATABA MPYA UNITED



JUAN MATA AANZA MAZUNGUMZO YA KUSAINI MKATABA MPYA UNITED
HATIMAYE kiungo kutoka nchini Hispania, Juan Mata ameanza kupata mwangaza wa maisha yak echini ya utawala wa meneja wa Manchester United, Jose Mourinho kufuatia hatua ya kuwa katika mazungumzo ya kusaini mkataba mpya.

Mata ambaye alikuwa sehemu ya kikosi cha Hispania kilichotwaa ubingwa wa Dunia wakati wa fainali za Kombe la Dunia mwaka 2010 ameonyesha kuwa tayari kubaki Old Trafford na kucheza soka la ushindani kwa vitendo.

Kiungo huyo mwenye miaka 28, kwa sasa bado ana mkataba wa miaka miwili ambao unamwezesha kulipwa mshahara wa pauni 130,000 kwa juma, na kama mambo yatakwenda vyema kiasi hicho cha fedha kitaongezeka.

Mata ambaye aliwahi kucheza soka akiwa na klabu ya Valencia kabla ya kuelekea nchini Uingereza kujiunga na Chelsea na kisha Man United, alionekana kuwa adui mkubwa wa Jose Mourinho na ujio wa Meneja huyo ulitazamwa kwa jicho la tatu kwa kuamini huenda ulikuwa mwisho wa kiungo huyo.

Mourinho amethibitisha kuendelea kwamazungumzo baina ya Man United dhidi ya mchezaji huyo na wakati wowote mambo huenda yakawa sawa.

"Kuna mazungumzo yanaendelea kati yake na uongozi na nina matarajio makubwa ya kuona jambo hilo likifanikiwa."


"Ameonyesha nia ya dhati ya kutaka kubaki hapa kwa vitendo kutokana na kutumia nafasi ya kucheza soka safi kwa kufuata maelekezo anayopewa wakati wote," alisema Mourinho.


Comments