GEORGINIO WIJNALDUM AAHIDI KUISAIDIA LIVERPOOL KUIPOKONYA LEICESTER UBINGWA WA LIGI KUU



GEORGINIO WIJNALDUM AAHIDI KUISAIDIA LIVERPOOL KUIPOKONYA LEICESTER UBINGWA WA LIGI KUU
SI dhambi kuanza ubashiri mapema. Unapoona kuna neema inaanza kunyemelea milango yako, wewe tabiri tu.

Mchezaji mpya wa kikosi cha Liverpool, Georginio Wijnaldum anatarajiwa kuwa katika kikosi cha kwanza cha Liverpool.

Mchezaji huyo amesema kwamba anajua ameingia katika kikosi cha "Wekundu" hao wa Uingereza kwa ajili ya kazi moja tu ambayo ni kuisaidia Liverpool kuwa mabingwa.

Mchezaji huyo mpya katika kikosi hicho amesema kwamba anafahamu wajibu wake kwa kikosi hicho lakini si yeye pekee kama Georginio Wijnaldum anayeweza kuifanyia maajabu Liverpool.

Hata hivyo amesema kwamba kwa ushirikiano wa wachezaji wenzake, wanaweza kufanya kile kilichofanywa na Leicester City katika msimu uliopita.

Liverpool imekuwa ikiishia katika nafasi ya Top 4 katika Ligi Kuu, mafanikio ambayo Wijnaldum amesema si ya kujivunia tena na kinachotakiwa sasa ni kuwa mabingwa.

"Ni kweli tunaweza kukumbana na changamoto nyingi, lakini hii ndio soka yenyewe," amesema Wijnaldum akikaririwa na gazeti la Liverpool, Echo.

"Kama unacheza kwenye klabu kubwa kama Liverpool, mara zote unatakiwa kuwa na matumaini mapya, lakini hakuna jambo jema kama kushinda ubingwa."

Amesema: "Huwezi kukaa katika klabu kwa miaka minane au tisa bila kuipa ubingwa, halafu ukasema umeipa mafanikio. Kwangu mimi nimekuja kufanya kazi ya maana hapa."

Amesema, ndoto yake kwa Liverpool ni kusaidia kupata ubingwa na kwamba anataka iwe hivyo kwa msada wa wachezaji wenzake.

"Kama Leicester City imefanya hivyo kwanini sisi tushindwe?" amehoji Wijnaldum mwenye thamani ya pauni mil mil 23.

Alijiunga na klabu hiyo akitokea Newcaste United na amejihakikishia namba katika kikosi cha kocha Jurgen Klopp.

"Mimi najiamini sana. Kama mchezaji umefunga mabao 10 katika msimu mmoja ni hatua moja, lakini kama unajiunga na timu yenye watu wanaotamani kufunga zaidi, hiyo nayo ni hatua nyingine," amesema.

"Nimekuwa nikifunga. Nimefanya hivyo katika klabu za Feyenoord, PSG na Newcastle. Muda wote natamani kufunga, ndicho kipaji changu. Liverpool nimekuja kwa kazi moja tu ya kufunga, kwasababu nina kiwango bora cha kufunga."


Amesema kwamba nayasema hayo kwasababu anataka kuapia kwamba hakuna sababu ya kukosa kuisaidia klabu yake mpya.


Comments