UFINYU WA MABAO WAIKABILI COPA AMERICA KWA MITANANGE YA AWALI



UFINYU WA MABAO WAIKABILI COPA AMERICA KWA MITANANGE YA AWALI
Usiku wa kuamkia leo, mitanange mitatu ilikanyagwa katika viwanja 3 tofauti.

Mchezo wa kwanza uliwa shuhudia Peru wakiwafunga Haiti goli 1-0. Kipindi cha kwanza hakikuwa na goli ingawa Peru walimiliki zaidi mpira hasa katikati ya uwanja wakitumia mfumo wa 4-4-2 na kuwabana Haiti ambao wao walitumia mfumo wa 4-3-3.

Iliwachukuwa Peru mpaka dakika ya 66 kujipatia bao lao lililowekwa kimiani na mshambulizi hatari Paolo Guerrero kwa kichwa cha kuchumpa kufuatia krosi mujarabu iliyotumwa na Edson Flores na kumshinda golikipa Johny Plaside wa Haiti. Haikushangaza Guerrero kufunga bao hili kwani ikumbukwe kuwa huyu ndiye mfungaji bora wa mashindano haya kwa misimu miwili iliyopita.
COSTA RICA vs PARAGUAY

Wengi walitarajia kuwa mpambano huu utakuwa wa mbinu za kutafuta mabao pamoja na ufundi mkubwa, lakini tofauti yake ikawa ni mtanange wa nguvu zaidi na kukamiana, kitu kilichopelekea mwanuzi kugawa kadi kama njugu, kwani alitoa kadi za njano kwa wachezaji 5 kadi nyekundu kwa mchezaji wa Costa Rica Kendall Waston mnamo dakika ya 94.

BRAZIL vs EQUADOR

Katika kipute hiki matokeo yalikuwa ni kutofungana (0-0), lakini ukweli ni kuwa huu ulikuwa ni mchezo uliokuwa wa kuburudisha (very entertaining) kuliko michezo mingine yote iliyokwisha kuchezwa hadi sasa. Kwa upande wa Brazil waliotumia mfumo wa 4-2-1-2-1 na kuwatumia zaidi Willian Coutinho kuchezesha timu, walipeleka sana mashambulizi langoni mwa Equador lakini kipa wa Equador aliweza kuokoa hatari zote.

Mnamo dakika ya 66 ya mchezo, mchezaji hatari wa Equador Miller Balanos alimpita golikipa wa brazil pembeni ya lango na kuuweka mpira kimiani, lakini mwamuzi alilikataa bao hilo kwa madai mpira ule ulikuwa umetoka kabla mfungaji hajaitia kambani. Hivyo mpaka mwisho matokeo ni 0-0.

Leo usiku kuamkia kesho

JAMAICA vs VENEZUELA (Soldier Field)
MEXICO vs URUGUAY (Phoenix Stadium)


Comments