PEDRO: SIJUTII KUJIUNGA CHELSEA ILA BADO NAIKUMBUKA BARCELONA YANGU


PEDRO: SIJUTII KUJIUNGA CHELSEA ILA BADO NAIKUMBUKA BARCELONA YANGU
WINGA wa Chelsea, Pedro amesema kwamba hajutii kujiunga na klabu hiyo ya Stanford Bridge, lakini akakiri akisema kwamba anaikumbuka Barcelona.

Staa huyo wa timu ya taifa ya Hispania, alisajiriwa na Jose Mourinho Agosti, mwaka jana na kwa haraka akaweza kung'ara katika michuano ya Ligi Kuu England kwa kufunga bao katika mechi yake ya kwanzakatika mchezo walioibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Westbrom.

Baada ya kufunga mabao hayo, straika huyo mwenye umri wa miaka 28 alionekana kama angetamba zaidi lakini badala yake akajikuta akifunga mabao saba katika mechi 29 alizocheza Chelsea.

Hata hivyo, Pedro anakiri kuikosa klabu yake iliyomlea, Barca na huku akisema kuwa msimu uliopita ulikuwa mgumu kwake, lakini akaendelea na msimamo wake wa kwamba alifanya uamuzi sahihi kwa kujiunga na Chelsea.

"Ulikuwa ni mwaka mgumu kwa kila mmoja wetu," staa huyo aliliambia jarida la Mundo Deportivo.

"Kilikuwa ni kipindi kigumu ikizingatiwa ndio kwanza ilikuwa nimewasili nikiwa na matarajio ya kwamba kila kitu kitakwenda vizuri, nilipata bao katika mechi yangu ya kwanza lakini baadae kila kitu kikaenda kombo," aliongeza staa huyo.


Alisema kwamba, walijaribu kujituma lakini kila kitu kikabadilika kuanzia hapo.


Comments