HUU ni ushauri tu ambao ni juu ya wenyewe, Manchester            United kuukubali ama kuupotezea. 
        Katika kinachoaminika kutaka kuona United ikirejea            katika kiwango chake cha zamani, Mashetani Wekundu hao            wameshauriwa kumsajili kiungo wa Leicester City, Danny            Drinkwater. 
        Ushauri huu umetolewa na aliyewahi kuwa kocha msaidizi            wa Manchester United, Rene Meulensteen.
        Kwa mujibu wa Meulensteen, kiungo huyo wa Mabingwa wa            premier msimu huu, Leicester City amewahi kupita Old Trafford            kama mchezaji kinda ambaye kwa sasa ni kati ya wachezaji            wanaoweza kuirejesha katika uimara United katika msimu ujao.
        Kocha huyo alisema kuwa, United wamekosa wachezaji wa            aina ya Drinkwater ambao wakipatikana na wengine, watairudisha            timu katika mazingira ya kuwa tishio kama ilivyo enzi ya kocha            Alex Ferguson.
        "Kama ukitaka kuichambua Leicester City na sababu            iliyochangia kutwaa ubingwa, huwezi kukosa kutaja kuimarika            kwa idara yao ya kiungo iliyoongozwa vyema na Drinkwater."
        "Kwangu mimi kama kocha, ninaamini kiungo huyo alikuwa            ndie bora na aliyechangia ubingwa wa The Fox na kwamba United            wanaweza kuimarisha kikosi cha msimu ujao kwa kumnyakua,"            alisisitiza Meulensteen.
        Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 26 ni zao la United            kwani ametokana na mradi wa kulea na kuibua vipaji ndani ya            Old Trafford lakini alishindwa kupata mafanikio na kuamua            kutimkia Leicester City mnamo Januari, 2012.
        Tangu hapo Drinkwater amekuwa katika uhakika wa            kutumika katika kikosi cha kwanza cha mbweha hao wa King Power            na hadi msimu huu alipong'ara na kuipa ubingwa.
        Kiwango chake cha msimu huu kimemuwezesha pia kuitwa            katika kikosi cha timu ya taifa ya England kitakachoshirika            michuano ya mataifa ya Ulaya itakayofanyika nchini Ujerumani.
        Meulensteen bado anasisitiza kuwa United wana nafasi ya            kumrejesha Drinkwater katika viunga vya Old Trafford na kuwa            msaada wa timu msimu ujao.
        "Drinkwater bado ana historia ndani ya Manchester            United kwasababu ni zao lao na wakati wa kufanya hivyo ni            sasa."
        "Wakati mwingine lazima klabu iangalie wapi ilipokosea            na kutafuta njia ya kujiimarisha, kipindi hiki sio cha            kuangalia zaidi wachezaji wa kigeni kwasababu wanahitaji muda            mwingi wa kujiweka sawa."
        
Comments
Post a Comment