DALEY BLIND AMLILIA MHOLANZI MWENZAKE LOUIS VAN GAAL... asema alistahili kupewa muda zaidi Old Trafford
DALEY Blind              amesema amefadhaishwa na kutimuliwa kazi kwa Louis Van Gaal              akiona kwamba kocha huyo Mholanzi mwenzake hakupewa muda wa              kutosha madarakani Manchester United.
        Van Gaal              alitimuliwa Jumatatu hii, siku mbili tu baada ya kuiongoza              klabu hiyo kutwaa taji la kwanza, Kombe la FA, tangu utawala              wa Sir Alex Ferguson ulipomalizika mwaka 2013.
        Blind alisajiliwa              na Van Gaal Manchester United kwa ada ya uhamisho wa pauni              mil 14 akitokea Ajax mwaka 2014 na anaamini kwamba Mholanzi              mwenzake alistahili kupewa muda zaidi wa kuweka mawazo yake              Old Trafford.
        "Daima nimekuwa              nikifanya kazi vyema nae na natamani ushirikiano huu              ungeendelea kwa muda mrefu zaidi," Blind aliwaambia              waandishi wa habari katika kambi ya timu ya taifa ya              Uholanzi nchini Ureno.
        "Kocha katika              klabu kubwa kama England, ni kawaida kuwa katika presha,              lakini katika kipindi cha miezi sita iliyopita hakuwa              akitendewa haki. Nadhani makocha kama Louis Van Gaal ambao              wameshinda mataji mengi, wanastahili kuheshimiwa zaidi."
        
Comments
Post a Comment