MAURICIO Pochettino "anawapasua kichwa"            mabosi wa Tottenham kutokana na kuchelewa kusaini mkataba            mpya.
        Spurs inataka kumalizana haraka na kocha            huyo kutokana na hofu kuwa anaweza kwenda Manchester United            baada ya Paris Saint-Germain kujiunga katika kumuwinda Jose            Mourinho anayetarajiwa kumrithi Louis van Gaal kiangazi                hiki.
        Barcelona na Real Madrid nazo pia            zinatajwa kummezea mate kocha huyo baada ya kuibadili Spurs            kuwa timu ya kutisha Ulaya katika kipindi cha misimu miwili.
        Spurs wamekuwa wakimsubiri kwa wiki kadhaa            sasa Pochettino kutia saini mkataba wa miaka mitano wenye            thamani ya pauni milioni 5 na bonasi.
        Pochettino ambaye bado ana zaidi ya miaka            mitatu katika mkataba wake wa sasa aliosaini mwaka 2014,            alisema mwezi huu kuwa anataka kubaki Spurs.
        Lakini akasema hana muda wa kujadili            mkataba kwa sasa, kwa sababu hataki "kuvurugwa" katika            harakati zake za kuipa Spurs taji la kwanza tangu 1961.
        Hata hivyo, mabosi wa klabu hiyo wanaamini            Pochettino mwenye umri wa miaka 44, ana uwezekano wa kusaini            mkataba, lakini wakakiri kuwa kuchelewa kwake kunawaweka            katika hali ya wasiwasi.
        
Comments
Post a Comment