JOSE MOURINHO amejikuta akiwa njia panda kuhusu mustakabali wake Manchester United, na sasa ameitaka klabu hiyo kumuhakikishia kwa maandishi kama atakuwa kocha wao msimu ujao.
Baada ya Manchester United kuonekana kuchelewa, sasa Real Madrid inajipanga kumnyakua kocha huyo iwapo Zidane atashindwa kuivusha timu hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa.
Mtaalamu huyo raia wa Ureno, yuko nje ya kazi tangu alipoondoka Chelsea Desemba mwaka jana, na tangu wakati huo amekuwa akisubiri kuitwa rasmi Old Trafford.
Hata hivyo, Mourinho ana ahadi ya mdomo kutoka katika klabu hiyo, na inaonekana uwezekano wa ajira yake kuwa shakani baada ya kocha wa zamani wa United, Sir Alex Ferguson kujitosa kumuunga mkono kocha wa sasa, Louis van Gaal.
Kwa mujibu wa The Sun, Mourinho mwenye umri wa miaka 53, sasa anaitaka United kumuhakikishia kibarua kwa maandishi, ili aweze kuanza kwa ukamilifu maandalizi kwa ajili ya msimu ujao.
Real Madrid ilitaka kumchukua Mourinho dirisha dogo la usajili baada ya kumtimua Rafa Benitez, lakini ikarudisha majeshi baada ya kubaini kuwa kocha huyo tayari ameelekeza akili yake Old Trafford.
Lakini sasa baada ya kuona United imekuwa 'slow' Real Madrid imeanza tena kupiga hesabu za kumrejesha Mourinho aliyewapa taji pekee la La Liga ndani ya miaka minane.
Kumekuwa na mchanganyiko wa habari katika siku za karibuni juu ya hatima ya Van Gaal, ambapo wachezaji wanaelezwa kutaka atimuliwe wakati vyanzo vingine vikipasha kuwa kibarua chake kipo salama.
Comments
Post a Comment