WAKALI WATANO WA AMERIKA YA KUSINI WANAOONGOZA KUTIKISA NYAVU EPL


WAKALI WATANO WA AMERIKA YA KUSINI WANAOONGOZA KUTIKISA NYAVU EPL

America

Mchezo wa soka umekuwa ni kama utamaduni na kazi kwa nchini nyingi za Amerika ya Kusini hasa Brazil, Argentina, Uruguay, Chile, Peru, Mexico, Paraguay na nyingine nyingi.

Amerika ya Kusini imewahi kutoa wachezaji wenye majina makubwa kama vile Pele, Maradona, Ronaldo, Messi ambaye bado ni mwiba kwa sasa.

Katika maeneo mbalimbali kama shuleni, mitaani, viwanja vidogovidogo na kwenye fukwe huko Amerika ya Kusini utawakuta watu wakikusanyika na kushindana kuonesha ujuzi wao wa kuuchezea mpira.

Kwa mafano kwenye mitaa mbalimbali ya jiji la Rio de Janeiro huko Brazil, utawaona vijana wakishindana kucheza soka pekupeku kuanzia asubuhi kunapokucha mpaka jua linapozama katika viwanja ambavyo havina ubora huku vilevile mipira wanayochezea ikikosa ubora.

Kwa kufanya hivyo, hali hii hupelekea kuwa na viwango vikubwa na baadye kusajiliwa na timu kubwa ulimwenguni na kuwa wachezaji wenye majina makubwa duniani hasa sehemu za Ulaya ambapo mpira unalipa kupindukia.

Ligi Kuu nchini England imekuwa ikipokea wachezaji wengi kutoka Amerika ya Kusini hasa washambuliaji. Wengi wao wamekuwa wakicheza kwa mafanikio kutokana na uwezo wao mkubwa wa ama kuwasumbua mabeki au kupachika mabao.

Sasa hapa nawatupia jicho washambuliaji 5 kutoka Amerika ya Kusini ambao wamewahi kuwa vinara wa mabao EPL.

5. Nolberto Solano-magoli 49

America 1

Solano alikuwa ni mchezaji wa kwanza kutoka Peru kucheza kunako Ligi kuu ya England baada ya kusajiliwa na Newcastle United mwaka 1998 akitokea klabu ya Boca Juniors. Alicheza klabuni hapo kwa vipindi viwili na kufunga mabao 37 katika michezo 240.

Kiungo huyo wa zamani wa Peru pia alicheza Aston Villa ambapo alicheza michezo 48, akifunga mabao 8 na vile vile West Ham United mwaka 2007-08 na kufunga mabao 4 katika michezo 23.

4. Gus Poyet-magoli 54 

America 2

Poyet alielekea Premier League mwaka 1997 akitokea kunako klabu ya La Liga ya Real Zaragoza akijiunga na Chelsea ambapo alifanikiwa kufunga mabao 36 ndani ya michezo 105.

America 3

Meneja huyo wa zamani wa Sunderland, badaye alihamia Tottenham mwaka 2001 na kufunga mabao 18 katika michezo 82 kabla ya kuamua kutundiga daluga.

3. Luis Suarez-magoli 69

America 4

Huyu alidumu katika klabu ya Liverpool kwa misimu minne na kufunga mabao 69.

Alijiunga na Liverpool mwaka 2010 akitokea kunako klabu ya Ajax ya Uholanzi. Alishinda tuzo ya mchezaji bora wa mwaka mara moja, tuzo ya PFA ya mwaka na kutwaa tuzo ya mfungaji bora wa Ulaya mwaka 2014.

Ni mchezaji pekee katika hostoria ya EPL kufunga 'hat-tricks' tatu dhidi ya klabu moja ambayo ni Norwich City.

2. Carlos Tevez-magoli 84

America 5

Tevez ni moja ya wachezaji wachache kuweza kucheza klabu mbili za jiji la Manchester kwa nyakati mbili tofauti na kufanikiwa kufunga mabao 84 katika EPL.

Alifunga mabao 7 kwenye michezo 26 wakati akicheza West Ham United kabla ya kujiunga na Manchester United na kufunga mabao 19 kwenye michezo 63.

America 6

Baadaye mwaka 2009, Tevez alihamia klabu ya Manchester City na kufunga mabao 58 kwenye michezo 113 kwa misimu minne aliyodumu klabuni hapo.

1. Sergio Aguero-magoli 94

America 7

Sergio Aguero, ambaye kwa sasa ni moja ya washambuliaji bora duniani, alimzidi Muargentina mwenzake Novemba 2015 alipofunga goli dhidi ya Liverpool katika dimba la Etihad.

Mshambulizi huyu wa zamani wa Atletico Madrid anaweza kufunga magoli zaidi endapo tu ataamua kuendelea kubaki Ligi Kuu England.

Aguero kwa sasa ameshadumu klabuni hapo kwa misimu minne.

Alijiunga na Man City mwaka 2011 akitokea klabu ya Atletico Madrid.



Comments