KASI YA XABI ALONSO UWANJANI YAZUA SHUTMA KIBAO


KASI YA XABI ALONSO UWANJANI YAZUA SHUTMA KIBAO

KIUNGO wa Bayern Munich, Xabi Alonso amejikuta katikati ya shutuma kwamba amekuwa akicheza kwa  taratibu sana kipindi chote cha maisha yake ya soka, na akawajibu kwa masihara wapinzani wake akisema kwamba anataka majina na anuani zao ili aweze kuwafuatilia, akiamini ataweza kuwakamata!

Alonso ambaye ameshinda Kombe la Dunia, Euro mara mbili, Champions League mara mbili na mataji matatu ya ligi miongoni mwa medali kibao alizobeba, amekuwa akikabiliana na upinzani kuhusu kasi yake dimbani kwa miaka kadhaa sasa.

Miongoni mwa wasiopendezwa na kasi ya Alonso dimbani ni Claudio Ranieri aliyejitokeza mbele ya umma na kudai kwamba aliachana na mpango wa kumsajili kiungo huyo Juventus mwaka 2008 kutokana na kasi yake ndogo dimbani.

Wakati mtandao wa Goal ulipomwelekezea tuhuma hizo, Alonso mwenye umri wa miaka 34, alijibu kwa masihara: "Nipe majina yao. Nipe majina na anuani zao!" Akaendelea: "Sikuwa na haraka nilipokuwa na miaka 20 na sina haraka sasa, hivyo si kwenda naelekea kubadilika.

"Umri wangu haujalishi. Baadhi ya wachezaji wana umri wa miaka 28 na baadhi ya wachezaji wanaonekana vijana katika umri wa miaka 36. Yote ni kuhusu utendaji wao na umri wao unaweza kuwa udhuru tu.

"Unatakiwa kujua vipi unajisikia na hadi sasa mimi najisikia vizuri, ndiyo maana naendelea kucheza kwa kiwango cha juu. Kama ningefeli nisingalikuwapo hapa."


Comments