AZAM KUITOA BIDVEST WITS NA SIRI ILIYOFICHIKA NYUMA YA PAZIA


AZAM KUITOA BIDVEST WITS NA SIRI ILIYOFICHIKA NYUMA YA PAZIA

Azam vs Wits 5

Jumapili iliyopita Azam FC iliwashangaza wapenzi wengi wa soka la Bongo si tu kwa kuitoa kwenye mashindano ya kombe la Shirikisho barani Afrika Bidvest ambayo ni timu ngumu ya Afrika Kusini kwa jumla ya magoli 7-3, bali namna ambavyo Azam iliruhusu kufungwa magoli mengi kwenye mchezo wa marudiano ikiwa kwenye uwanja wake wa nyumbani tofauti na mchezo wa kwanza ambao Azam ilishinda kwa magoli 3-0 ikiwa ugenini.

Azam ikiwa nyumbani ilishinda kwa magoli 4-3 ikiwa imekubali kufungwa magoli sawa na yale ambayo ilifunga ikiwa ugenini kwenye mchezo wa kwanza.

Wengi hawafahamnu kwamba, kikosi cha Bidvest kilichocheza mechi dhidi ya Azam kwenye mchezo wa kwanza ni tofauti kabisa na kile kilichocheza kwenye mchezo wa marudiano jijini Dar es Salaa. Kwenye mchezo wa Awali uliochezwa Afrika Kusini, Wits walipumzisha karibu wachezaji wote wa kikosi cha kwanza na baadhi ya wachezaji wa akiba kwasababu ya kusubiri mchezo wao wa ligi ya kwao dhidi ya Orlando Pirates na wakachezesha wachezaji wengi wa academy dhidi ya Azam.

Wanafanya hivyo kwasababu wako katika mbio za kuwania ubingwa wa PSL ambako wapo nafasi ya pili wakiwa na pointi 48 baada ya kucheza mechi 23 pointi nne nyuma ya S'downs vinara wa ligi hiyo wenye pointi 52 wakiwa wamecheza michezo 23 pia.

Taji la ligi ya Afrika Kusini linashabihiana thamani na lile la michuano ya Afrika ndiyo maana Wits wameamua kuelekeza nguvu zao nyingi huko ambako wako kwenye nafasi nzuri ya kuibuka mabingwa kuliko kwenye michuano ya Afrika ambayo watatumia gharama kubwa lakini wakiwa hawana matumaini ya kutwaa taji.

Kwahiyo mchezo wa ligi dhidi ya Orlando Pirates ulikuwa ni muhimu kwao kuliko wa michuano ya Afrika dhidi ya Azam ndiyo maana wakawapumzisha nyota wao wa kikosi cha kwanza wasicheze dhidi ya Azam ambapo walifungwa magoli 3-0 kwenye uwanja wao wa nyumbani na kuwapanga dhidi ya Orlando Pirates kisha kufanikiwa kupata ushindi wa bao 1-0.

Azam kuruhusu mabao nyumbani

Ukiangalia wachezaji kama Henrico Botes, Siyabonga Nhlapo, ni baadhi ya wachezaji ambao hawakucheza kwenye mechi ya kwanza dhidi ya Azam iliyochezwa Afrika Kusini. Lakini wachezaji hao wamecheza mechi ya pili ya Dar, wachezaji wote waliofunga magoli matatu wa kikosi cha kwanza wote hawakucheza mechi ya kwanza.

Bidvest walichezesha academy siyo kikosi cha pili wakati huo kwenye akili zao wakiwa wanaiwaza mechi yao ya ligi ya nyumbani (PSL) ambayo walikuwa wanacheza dhidi ya Orlando Pirates. Kwahiyo waliamua kuwapumzisha wachezaji wao wengi wa kikosi cha kwanza na baadhi ya wachezaji wa kikosi cha pili kwa ajili ya mchezo dhidi ya Orlando Pirates ambao walishinda kwa bao 1-0 na wanashika nafasi ya pili kwenye ligi.

Baada ya kucheza mechi dhidi ya Orlando wakaja baadhi ya wachezaji ambao hawakucheza mechi ya kwanza dhidi ya Azam na imeonekana tofauti kati ya mchezo uliochewa Johanesburg na Dar. Mchezo wa Dar umekuwa na upinzani hata ukiangalia kwa upande wa Azam na wenyewe walifanya mabadiliko kidogo, Kipre Tchethe hakuheza mchezo wa kwanza lakini amecheza Dar na kufunga hat-trick, Alan Wanga hakucheza pia mchezo wa awali lakini amecheza mechi ya marudiano.

Magoli waliyofungwa Azam na Bidvest Wits

Nafikiri tuwasifie Bidvest kwa namna walivyofunga magoli yao, waliweza kutumia mapungufu ya mabeki wa Azam ambayo yalikuwa yanajitokeza hasa baada ya kuwa wameingia wachezaji watatu.

Wafungaji wa mabao yote matatu ya Bidvest ni wachezaji ambao hawakucheza mechi ya kwanza ukianza na Jabulani Shongwe,  Henrico Botes ambao ni wachezaji wanaotumiwa mara kwa mara kwenye kikosi cha kwanza cha Bidvest.

Kama umeangalia mechi zote mbili ambazo Azam wamecheza dhidi ya Bidvest kuanzia ya mechi ya Afrika Kusini na ile ya Dar, wachezaji wengi ambao wanategemewa kwenye kikosi cha kwanza hawakucheza mechi ya kombe la Confederation dhidi ya Azam. Sasa unaweza ukajiuliza maswali hapo kwnini hawakucheza wachezaji wa kutegemewa kwenye mashindano makubwa?

Nafikiri wao wanaipa kipaumbele ligi yao ya Afrika Kusini na hata kocha Gavin Hunt ukimsikia unagundua kwamba alikuwa anaomba timu yake itolewe kwenye mashindano hayo ili waweze kuweka nguvu zao zote kwenye ligi ya kwao Afrika Kusini.

Kwahiyo yale magoli waliyokuwa wakiifunga Azam hayakuwa mepesi, bali yalitokana na wachezaji wao wenye uwaezo wa juu ambao waliingia tofauti na wachezaji wao wa academy ambao walitoka na kuwapisha wazoefu.

Sasa jaribu kujiuliza kama wangekuwepo wachezaji kama Daine Klate winga wa zamani wa Orlando Pirates na Bafanabafana, angekuwepo Elias Pelembe winger maarufu sana Tanzania ambaye ni mchezaji wa Msumbiji na angekuwepo pia mfungaji bora wa Bidvest kwenye ligi ya kwao James Keene raia wa Uingereza ambaye hajacheza mechi zote mbili.

Kwahiyo Bidvest kwa matokeo waliyoyapata kwa mtazamo wangu ni kwasababu hawakuweka mbele umakini kwenye mechi ya Confederation ukilinganisha na ligi ya kwao.

Azam vs Esperance

Kwenye mchezo wa soka lolote linaweza kutokea, lakini katika hali ya kawaida ikija kwenye ukweli lazima tuwe wakweli, Azam inakwenda kukutana na timu ngumu.

Esperance kutoka Tunisia wote tunaifahamu husan kwenye hizi harakati za mashindano ya vilabu bingwa Afrika. Wao hawana masihara kama timu za Afrika Kusini, hawana kawaida ya kupumzisha wachezaji wanaweka full 'mziki'.

Kwahiyo changamoto iliyopo ni namna gani watakabiliana nao kwa kikosi walichonacho, Azam wanawachezaji wengi wazuri. Ukiangalia mchezaji kama Ramadhani Singano anazidi kuimarika kila siku zinavyokwenda, Kipre Tchetche mchezaji anayejituma sana na kupambana uwanjani, mchezaji kama John Bocco anaweza kutumia nafasi anazozipata.

Ukija kwenye eneo la katikati unakutana na Sure Boy, Himid Mao mchezaji ambaye anajitolea kwa kiasi kikubwa, Jean Mugiraneza 'Migi', Frank Domayo mchezaji ambaye hapati nafasi mara nyingi lakini ni mchezaji ambaye anakiwango kikubwa.

Kwahiyo ukubwa wa kikosi cha Azam walichonacho wakifanya maandalizi mazuri wanaweza wakatoa ushindani kwa Esperance lakini haitakuwa mechi nyepesi ni mechi ngumu.



Comments