MSEMAJI WA AFRICAN SPORTS AJIUZULU AKIDAI TIMU IMEJAA ‘VIHIYO’



MSEMAJI WA AFRICAN SPORTS AJIUZULU AKIDAI TIMU IMEJAA 'VIHIYO'

African Sports 1

Baada ya kujiuzulu mwenyekiti wa klabu ya African Sports ya Tanga, mkuu wa idara ya habari na mawasiliano wa klabu hiyo Muhasham Hatibu ameibuka na kukiri klabu yaop inamatatizo mengi ya kiutawala na kusema kujiuzulu kwa mwenyekiti wao ni pigo kwenye klabu yao.

"Kwenye timu yetu kuna majungu, fitna na figisu za hapa na pale yapo mengi lakini mengine hayapaswi kuwekwa kwenye vyombo vya habari. Kwahiyo naona hatua aliyochukua mwenyekiti bado naona amechelewa kuchukua, tarehe 15 siku moja kabla ya mechi yetu dhidi ya Coastal Union mwenyekiti alitaka kutangaza kujiuzulu watu wakamsihi asifanye hivyo".

"Kuna watu wanataka kupata madaraka zaidi ya yale waliyokuwa nayo, kuna wakati niliwahi kuzungumzia juu ya hilo wakanihisi vibaya lakini kwe klabu yetu kuna mikingamo na figisu hakuna mgawanyiko wa madaraka kila mtu anataka kuwa mkubwa inafikia wakati hadi wapenzi na wadau wanataka kuwa wakubwa kuliko mwenyekiti wao, sasa ikifika hapo uongozi wa timu unakuwa hauna kazi".

"Niseme ukweli kwamba, timu ya African Sports kwasasa inategemea nguvu za Mungu tu. Lakini timu ya African Sports hadi imefika hapo ni kutokana na nguvu za mwenyekiti binafsi. Hata gharama za timu inaposafiri ni yeye ambaye hutoa pesa zake mfukoni kwahiyo kujiuzulu kwa mwenyekiti kunaifanya timu ikose mtu muhimu sana kuliko maelezo".

"Kama ingekua kila mtu ndani ya African Sports  ameseoma na anajihesabu ni msomi, naamini kungekuwa na separation of power kusingekuwa na muingiliano wa majukumu kila mtu angefanya kazi kwa weledi. Lakini kwasababu hatufanyi hivi kuna watu wana watu hawako vizuri kwenye elimu yao kwenye klabu yetu ya African Sports".

Baada ya kuzungumza yote hayo ikafika muda muafaka ambapo msemaji wa wana-kimanumanu hao bila kuunga maneno akakisanua kwa kutangaza kujiuzulu wadhidfa wake kwenye klabu hiyo.

"Kuanzia leo mimi Muhashamu Hamad Hatibu ambaye nilikuwa nikijulikana kama afisa habari wa klabu ya African Sports najiuzulu rasmi, siyo tena afisa habari wa klabu ya African Sports", alimkaliza Hatibu.



Comments