Baada ya kocha msaidizi wa Yanga Charles Boniface Mkwasa kupewa mkataba wa kudumu na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wa kukinoa kikosi cha timu ya Taifa 'Taifa Stars' nafasi ya kocha msaidizi wa Yanga imebaki wazi na Fred Felix Minziro anatajwa kuchukua nafasi hiyo.
Mtandao huu baada ya kupata tetesi kuwa huenda Minziro akachukua nafasi ya Mkwasa kwenye kikosi cha Yanga ulimtafuta kocha huyo ili kutaka kujua kama taarifa hizo za yeye kuhusishwa kutua Jangwani kama zina ukweli wowote.
"Nawezakusema taarifa hizo zipo au hazipo lakini nasema yote kwa yote mimi popote pale naweza kufanya kazi endapo nahitajika", amesema Minziro.
"Nadhani hakuna asiyefahamu uwezo wangu kikazi ingawa kuna baadhi ya watu wasiolewa soka la Tanzania hawaelewi lilipotoka wamevamia na hawajui uwezo wangu lakini mimi najiamini uwezo wangu na kazi yangu nayoifanya kwahiyo popote mimi nafanya kazi".
"Tusubiri ndani ya siku mbili tatu nadhani tutapa jibu kamili", alimaliza Minziro ambaye leo anakutana na uongozi wa JKT Ruvu kujadili hatma yake ndani ya kikosi hicho.
Minziro amesema leo anatarajia kukutana na uongozi wa klabu ya JKT Ruvu kujadili hatma yake juu kibarua chake ndani ya klabu hiyo ambayo bado haijaonja ladha ya ushindi tangu kuanza kwa ligi (VPL) msimu huu wa 2015-2016.
Kumekuwa na taarifa nyingi kuhusu hatma ya Minziro ndani ya kikosi cha JKT Ruvu huku wengi wakisema kocha huyo huenda akaachana na maafande hao kufuatia matokeo mabovu ya mechi za mwanzo wa msimu huu baada ya kuingoza Ruvu kwenye vichapo vya mechi nne mfululizo.
Minziro hakusafiri na timu kuelekea Tabora kwenye mchezo dhidi ya Kagera Sugar uliomalizika kwa sare ya bila kufungana kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi wakati kikosi cha maafande hao kikiongozwa na kocha msaidizi Greyson Haule.
Minziro ni mchezaji wa zamani wa wanajangwani na ameshawahi kuwa kocha wa timu hiyo miaka kadhaa iliyopita.
Comments
Post a Comment