Hatimaye Wayne Rooney amevunja rekodi ya Sir Bobby Charlton ya kuwa mfungaji mwenye magoli mengi zaidi katika timu ya taifa ya England baada ya kutupia mpira wavuni kwenye ushindi wa 2-0 dhidi ya Switzerland ndani ya dimba la Wembley.
Katika mchezo huo wa kufuzu Euro 2016 Rooney alifunga katika dakika ya 84 na kufisha magoli 50, moja zaidi ya magoli 49 ya Sir Bobby Charlton.
Nahodha huyo wa England alifikia rekodi ya Sir Bobby Charlton Jumamosi iliyopita pale alipofunga kwa mkwaju wa penalti kwenye karamu ya bao 6-0 dhidi ya San Marino.
Jumanne usiku Rooney kwa kupitia tena mkwaju wa penalti, akafunga dhidi ya Switzerland na kuweka rekodi mpya England baada ya miaka 45.
Bao lingine la England lilifungwa na Harry Kane dakika ya 67.
Kwa ushindi huo, England imejihakikishia nafasi ya kwanza ya kundi E baada ya kushinda mechi zake nane na kujikusanyia pointi 24 na sasa hata ikipoteza michezo yake miwili iliyosalia, bado itakuwa kileleni kwa kundi hilo.
Comments
Post a Comment