KLABU za Yanga na            Simba zimesema, hazitakubali kucheza mechi zao za Ligi Kuu ya            Soka Tanzania Bara 'mchana', kama ambavyo wadhamini washiriki            wa Ligi hiyo, Azam Media wanavyoshawishi.
        Habari            zilizopatikana jijini Dar es Salaam zimesema kuwa, wadhamini            hao wapo katika mazungumzo na viongozi wa Shirikisho la Soka            nchini (TFF) pamoja na Bodi ya Ligi Kuu (TPLB) wakitaka mechi            za Ligi hiyo sasa zifanyike kuanzia saa 9:00 mchana ili kutoa            nafasi ya kuonyesha 'live' na baadae kituo hicho kuonyesha            michezo mingine ya Ligi ya Hispania.
        Akizungumza jijini            Dar es Salam jana, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa            Simba, Haji Manara alisema kuwa, Klabu yake haitakubali            kucheza mechi mchana kwasababu itaathiri katika kupata mapato.
        Manara alisema kuwa,            mbali na suala la mapato, pia kiufundi, kucheza mchana            kutawaumiza wachezaji wao kutokana na hali ya hewa ya jua            iliyopo Dar es Salaam tofauti na wanavyotaka kulinganisha na            baadhi ya mechi za Ulaya zinazochezwa mchana.
        "Klabu ya Simba            tunasema hatuko tayari kucheza mechi yoyote mchana,            tunashukuru kiasi wanachotupa Azam lakini haiwezi kutuumiza            kwa kubadili muda wa kuanza kwa mchezo, sisi sehemu kubwa ya            fedha tunazotegemea ni za mapato ya milango," alisema Manara.
        Manara alisema,            mechi zitakapochezwa mchana zitawaathiri kiuchumi na kiufundi,            kwasababu itabidi timu za vijana zichezwe saa 5:00 asubuhi na            kuwapa chakula cha mchana saa 4:00 asubuhi.
        Kiongozi huyo            aliwatahadharisha viongozi wa TFF na Bodi ya Ligi kulikataa            pendekezo hilo, kwasababu itawafanya wachezaji kuathiri            viwango kutokana na hali ya jua la Dar es Salaam linavyochoma.
        Naye, Katibu Mkuu wa            Yanga, Jonas Tiboroha alisema kuwa, ni vema kila jambo kabla            ya kufikia maamuzi, viongozi waahusishe wadau wao ambao ni            Klabu zinazoshiriki Ligi hiyo.
        Alisema kuwa, kwa            kufanya mazungumzo na kila upande na kufikia makubaliano, Ligi            itachezwa kwa ufanisi na kila upande utajiandaa na mazingira            husika.
        Mkuu wa Idara ya            Habari na Mawasiliano, Baraka Kizunguto alisema kuwa, ni kweli            kuna baadhi ya mechi zinazohusisha Klabu hizo zitakazochezwa            mchana na kuitaja mojawapo kuwa ni kati ya Yanga na Mgambo            JKT.
        Azam Media iliingia            mkataba wa miaka mitatu na TFF, kwa ajili ya kuidhamini Ligi            hiyo, wenye thamani ya sh. 5.56 Bil, wakati wadhamini wakuu,            Kampuni ya Vodacom mwaka huu walisaini mkataba mwingine wa            miaka mitatu wenye thamani ya sh. 6.9 Bil.
        Hata hivyo, Simba na Yanga pia            wanadhaminiwa na bia ya Kilimanjaro, wakati benki ya NMB            inaidhamini timu ya Azam.
        
Comments
Post a Comment