Na Shaffih Dauda
          Namshukuru Mungu aliyenivusha salama mwezi Julai na sasa          nimeanza safari ya kuipunguza Agosti! jambo la kuvutia ndiyo          mwezi ambao ligi ya England, Hispania na nyingine huanza!
          Juma hili nimekuwa nikifuatilia Kombe la Kagame linaloendelea          jijini Dar es salaam, sitazungumzia matokeo ya timu zote          kwasababu makala hii inawatazama zaidi Azam FC.
          Nimebahatika kuzitazama mechi zote za Azam za kundi C ikishinda          1-0 dhidi ya KCCA ya Uganda, 3-0 na Malakia FC ya Sudan Kusini          na mechi ya mwisho ikiichapa 5-0 Adama City ya Ethiopia.
          Pia niliwatazama katika mechi ya Robo fainali ambayo walishinda          kwa penalti 5-3 dhidi ya Yanga baada ya suluhu ndani ya dakika          90.
          
          Lengo la kuwafuatilia Azam kwa ukaribu ingawa sitazungumzia          matokeo yao ya nusu fainali iliyopigwa jana dhidi ya KCCA, ni          kuona kama mabadiliko makubwa ya mfumo wa uendeshaji wa timu          yameanza kuleta matunda.
          Mara nyingi nimekuwa nikiwapigia kelele Azam hasa wanapoleta          mambo ya 'kiswahili' , huku wadau wengi wa soka wakiamini ndiyo          klabu pekee inayoweza kulibadili soka la Tanzania.
          Mapema mwezi Juni mwaka huu, Azam walitangaza mfumo mpya wa          utawala wa klabu na kuunda vitengo vyenye watu wenye taaluma          husika, ambao tunaamini hawaingiliwi.
          kwa faida yako msomaji, Muundo wa uongozi wa Azam FC uko hivi:
          Bodi ya wakurugenzi: Hiki ni kikao cha juu kabisa cha maamuzi ya          klabu, wajumbe wake wamebaki kuwa wanafamilia wa familia ya          Bakhresa. Viongozi na baadhi ya watendaji hualikwa kwenye vikao          ili kutoa ripoti za utendaji na sera.
          Uongozi: Mwenyekiti wa klabu amebaki kuwa mzee Said Mohammed,          huku aliyekuwa katibu mkuu wa muda mrefu tangia klabu ianzishwe,          Nassor Idrissa "Father" akiwa Makamu Mwenyekiti. Nafasi ya          katibu mkuu ilifutwa. Nafasi ya Ukurugenzi wa Sheria na haki za          wachezaji imeendelea kushikiliwa na mwanasheria Shani Christoms.
          Watendaji: Mtanzania Saad Kawemba anaendelea kuwa Mtendaji Mkuu          wa klabu, huku klabu ikimuajiri Muingereza mwenye asili ya          Uganda, Eli Eribankya kuwa Meneja utawala na fedha. Eribankya          anasaidiwa na mchezaji wa zamani wa Azam FC Mtanzania, Lackson          Kakolaki.
Benchi la ufundi: Stewart John Hall kutoka Uingereza amerejea          kwa mara ya tatu kuongoza benchi la ufundi la Azam FC. Hall          anasaidiwa na Mganda George Best Nsimbe, huku Mark Philips          kutoka Uingereza akiwa kocha wa magolikipa. kocha wa magolikipa          aliyedumu kwa muda mrefu Iddi Abubakar anaendelea kuwepo kama          msaidizi wa Philips.
          Mtaalam wa tiba ya viungo na lishe "Team Physiotherapist and          Nutritionist" ni George Adrian Dobre kutoka Romania na Yusuf          Nzawila ameendelea kuwa Kit Manager.
          Benchi la ufundi la academy: Mario Marian Anton Marinica kutoka          Romania anaongoza benchi la ufundi la timu ya vijana akisaidiwa          na Mtanzania , Dennis Kitambi na Idd Nassor Cheche. Twalib          Mhidin anaendelea kuwa msaidizi wa Team Dr kwa vijana na mtunza          vifaa msaidizi vya vijana ni Saleh Sale.
Ukiangalia mfumo huu wa uongozi, Azam wanastahili pongezi kwasababu Stewart Hall na benchi lake la ufundi wanafanya wanavyotaka na hata ukiwatazama wachezaji wanavyocheza kwasasa unaona kabisa hawachezi kwa ajili ya mtu fulani, wanacheza kwa ajili ya benchi la ufundi.
Stewart sio kocha tu bali ni Meneja wa timu, hakika anatupa          maana halisi ya Wazungu ya Meneja wa timu.
          Meneja anawajibika kuwaongoza wachezaji kama kundi, pia          anawajibika 'kum-meneji' mchezaji mmoja mmoja, anatakiwa kujua          anahitaji nini, ana mapungufu gani na amsaidiaje ili kupata          kilicho bora kutoka kwake.
          Mfano mzuri ni wakati Arsene Wenger anajiunga na Arsenal mwaka          1996. Alikuta wachezaji wengi ni wazee wakiwemo Tony Adams,          David Seaman, Martin Keown, Mathew Upson, Ray Parlour, Ian          Wright na wengineo.
          Ili kupata kilicho bora kutoka kwao, Wenger kwa kushirikiana na          mtaalam wake vya vyakula ambaye Azam pia wanaye, aliwatengenezea          wachezaji 'Menu' ya kula ili waendelee kuwa na nguvu uwanjani.
          Wenger alikaa na wake wa wachezaji na kuwapa semina na ratiba ya          chakula kwa mcheza mpira, huwezi amini wale, 'wazee wa Arsenal'          walichukua ubingwa wa England msimu wa 1997/1998.
          Baada ya pale, Wenger akatengeneza falsafa yake, bodi ya          Ukurugenzi ikamwambia inataka nini na yeye akajua nini cha          kufanya ili Malengo yaweze kutimia nje na ndani ya uwanjani.
          Azam imekuwa mfano wa kweli katika hili, bila kugusia matokeo ya          Kagame, timu inaonekana kuwa na viongozi sahihi, wasioingiliana          kimajukumu na ndio maana wachezaji wanaonekana kuwa huru na          kucheza kwa maelekezo ya benchi la ufundi.
          Nawaasa Azam waendelea kubaki katika msingi huo na wamwamini          Stewart ambaye naamini hajawahi kuwa kocha mbaya zaidi ya          wapambe kumharibia kwa wenye timu.
          Tukutane Jumamosi ijayo panapo majaaliwa!
Makala hii imetoka jumamosi hii kwenye gazeti la Championi.
Comments
Post a Comment