MASHABIKI WA MBEYA CITY WAFUNGUA KAMPUNI ‘KUIPIGA TAFU’ TIMU YAO



MASHABIKI WA MBEYA CITY WAFUNGUA KAMPUNI 'KUIPIGA TAFU' TIMU YAO

Mbeya City Campany
Miezi michache baada ya kufungua akaunti  kwenye benki ya Posta Tanzania tawi la Mbeya, hatimaye mashabiki wa Mbeya City FC wamekamilisha usajili wa kampuni  ya mashabiki ambayo itakuwa inajushughulisha na masuala mbalimbali ya maendeleo kwa ajili ya timu yao.

 Mwenyekiti wa mashabiki hao Bwana Adam Simbaya amesema kuwa wameamua kusajili kampuni ili kuwawezesha kupata tenda mbalimbali ambazo zitakuwa vyanzo vya mapato ili kuwafanya mashabiki kuwa na nguvu ya pamoja katika kuichangia timu yao kwenye masuala mbalimbali  na pia kutoa ajira kwa baadhi ya mashabiki ambao kwa namna moja ama nyingine walikuwa hawana majukumu ya kufanya.

"Tayari tumeshasajili kampuni, lengo letu ni kuwa mashabiki wenye nguvu ya kweli kwa timu yetu, uwepo wa Mbeya City Fans Company LTD kutatuwezesha kupata tenda mbalimbali za ndani na nje ya timu yetu ambazo zitakuwa vyanzo vya mapato kwetu, kama mjuavyo sisi tunasafiri kwenda kuisapoti timu yetu mahala popote inapocheza, kuwa na kampuni kutatufanya kuiepuka michango ya kila mara kwa sababu tutakuwa na vyanzo vizuri na vyenye uhakika  vya mapato" alisema  Adam.

Akiendelea zaidi Mwenyekiti huyo alisema kuwa sasa wana uhakika tenda ya kuuza jezi na vifaa vingine vya timu itakuwa  yao pekee jambo litakaloongeza wigo wa kampuni yao kuwapatia ajira mashabiki ambao wamekuwa hawana majukumu  ya kufanya pindi wanapokuwa nje na ushabiki.

"Tunafahamu City ina mashabiki wengi, katika hili ni wazi si wote wenye majukumu ya kufanya nje ya ushabiki, kwa maana hiyo uwepo wa kampuni yetu utatoa fursa nyingi za ajira hasa ukizingatia tenda mbalimbali tutakazopata ndani na nje ya timu yetu, huku pia tukitarajia kutumia kile kinachopatika kuisaidia timu yetu kwenye masuala mbalimbali ikiwemo usajili, kambi na mengine", alisema.

Kampuni ya mashabiki hao wa City imesajiliwa kwa jina la Mbeya City Fans (MCF) Co LTD  na kwa kuanzia tayari imeshapewa tenda ya kuuza jezi na vifaa mbalimbali vya timu  kwenye msimu huu wa ligi kuu  Tanzania bara unaotarajia kuanzia mwezi  Agosti mwaka huu.

Uzinduzi wa kampuni hii ya mashabiki ambayo ni ya kwanza Tanzania umepangwa kufanyika tarehe 31/7/2015 kwenye ukumbi wa Mkapa Hall jijini Mbeya.



Comments