Okwi apiga hat-trick ya tatu VPL

Okwi

Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
'Tangu aanze kucheza Tanzania akitokea SC Villa ya kwao Uganda, Okwi alikuwa hajawai kufunga hat-trick katika michuano mbalimbali nchini Tanzania.'

HAT-trick aliyoifunga jana imeweka rekodi kwa kiungo mshambuliaji wa Simba, Mganda Emmanuel Okwi, ikiwa ni ya kwanza kwake tangu aanze kucheza soka Tanzania.

Okwi alikamilisha hat-trick yake dakika ya 50, Simba ilipolipa kisasi kwa kuifumua Mgambo Shooting Stars kutoka Kabuku, Handeni jijini Tanga mabao 4-0 katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) Uwanja wa Taifa.

Hat-trick hiyo imemfanya Okwi afikishe mabao 10 msimu huu wa VPL, ikiwa pia ni hat-trick ya tatu msimu huu wa ligi hiyo baada ya washambuliaji Ibrahim Ahibu wa Simba kupiga hat-trick pia katika mechi yao waliyoshinda 6-0 dhidi ya Prisons Februari 28 na Amissi Tambwe wa Yanga aliyefunga mabao manne katika ushindi wao wa 8-0 dhidi ya Coastal Union Machi 8.



Comments