‘ Sababu tatu muhimu kwanini Coutinho anacheza kikosi cha kwanza Yanga SC’


HMB_6496 

  Na Baraka Mbolembole, Dar es Salaam,

 Andrey Coutinho alihusika katika magoli yote matatu ya Yanga SC katika ushindi wa 3-0 ugenini dhidi ya mabingwa wa zamani wa Tanzania, Tanzania Prisons katika uwanja wa Sokoine, Mbeya. Nafasi unapoipata ni lazima uitumie na hicho ndicho anachofanya Coutinho tangu alipoondoka Marcio Maximo hadi sasa Mbrazil huyo amecheza michezo 11 mfululizo katika kikosi cha kwanza cha Yanga.

 Hans Van der Pluijm ametokeo kumuamini kiungo huyo wa mashambulizi na hakika nyota huyo hajamuangusha hata kidogo. Yanga imekuwa ikicheza mfumo wa 4-4-2 tangu kuwasili kwa Hans. Mwalimu huyo raia wa Uholanzi amemfanya Coutinho kuwa ' mtu wa mashabiki' hivi sasa kutokana na kiwango chake kizuri ambacho kimetokea kuwa msaada mkubwa kwa timu yake.

 Coutinho alikosa makali katika michezo saba ya mwanzo katika ligi kuu chini ya Maximo, lakini tangu aliponusurika kutemwa mwezi Disemba, 2014 kutokana na kuonesha kiwango cha chini katika mchezo wahisani wa ' Nani Mtani Jembe' uliomalizika kwa Simba SC 2-0 Yanga SC. Maximo hakuondelewa kwa sababu za matokeo, ukichunguza kwa umakini utagundua kuwa mkufunzi huyo Mbrazil alishindwa ' kuchezesha timu hiyo' licha ya kukusanya wachezaji wengi wenye uwezo wa kucheza katika mifumo tofauti. Kimazoea,

 Katika dakika ya tatu alipiga kona-pasi ambayo Msuva alifunga, dakika ya 11 akapiga kiki kali ambayo ilimgonga mchezaji wa Tanzania Prisons na kuifanya timu yake kuwa mbele kwa mabao mawili. Namzungumzia kijana-mtiifu ambaye ni ' tumaini maalumu' la kocha wa Yanga SC hivi sasa Hans Van der Pluijm si mwingine ni kiungo wa mashambulizi ( attacking midfield) Andrey Coutinho.

 Akiwa amecheza michezo 12 ya kimashindano ( saba ya ligi kuu, minne ya kombe la Mapinduzi na mmoja wa klabu bingwa Afrika) chini ya mwalimu Hans, kiungo huyo anayetumia mguu wa kushoto ametokea kuwa mchezaji ' siyegusika' katika kikosi cha kwanza. Licha ya kukutana na changamoto kubwa ya kupingwa na kuitwa ' mchezaji asiye stahili kuichezea Yanga' baada ya kucheza kwa kiwango cha chini katika mchezo wa hisani ' Nani Mtani Jembe' dhidi ya mahasimu wao wa soka nchini Simba SC, Coutinho, 25 alinusurika kutemwa katika dirisha dogo la usajili.

 Hans amekuwa akiiichezesha Yanga katika mfumo wa 4-4-2 na wakati mwingine amekuwa akiichezesha katika mfumo wa 4-3-3. Mara nyingi sana Countinho anacheza kama mshambulizi wa pili au kiungo-mshambulizi akitokea pembeni ya uwanja, inategemea na majukumu ambayo kocha wake humpatia. Inashangaa sana hadi sasa kumuona mchezaji huyo akicheza katika kikosi cha kwanza . Juhudi na maarifa yake vimemsaidia mno huku pia akiwa na uvumilivu hasa wa kiuchezaji kwa kuamini kuwa mchezaji mzuri ni Yule anayeisaidia timu yake ndani ya uwanja na si vinginevyo.

 Zifuatazo ni sababu TATU  muhimu ambazo zinachangia mchezaji huyo kucheza katika kikosi cha kwanza cha Yanga SC …….

 ' KIPAJI  HALISI'…..

 Majuzi nilikuwa nazungumza na ' kaka mkubwa' Shaffih Dauda na moja ya mazungumzo yake alikuwa akizungumzia kuhusu kipaji cha mtu, alisema kuwa ' kipaji pekee hakitoshi kumfanya mtu kufikia malengo yake', kujitoa sadaka ni jambo la lazima kwa mtu yoyote ambaye anaamini kuwa kipaji alichonacho kinaweza kuimarisha maisha yake na family kiujumla.

 Nani asiyejua kuhusu ' Brazil na soka'  Brazil inafahamika kama ' wafalme wa kandanda duniani' lakini si kila mchezaji anayetoka nchini humo na kucheza ng'ambo hupata mafanikio. Wakati Maximo aliporudi nchini kama mkufunzi wa Yanga katikati ya mwaka uliopita, aliambatana na wachezaji wawili ( coutinho na Geilson Santos ' Jaja'). Licha ya kipaji kikubwa cha ufungaji alichonacho mshambulizi Jaja alikosa nguvu na hamasa ya kuwashawishi wapenzi wa klabu yake kuwa yeye ni mchezaji mzuri.

  Jaja alijiondoa mwenyewe baada ya kucheza michezo nane ya kimashindano na kufunga magoli matatu. Coutinho alikosa nguvu lakini mara baada ya kuondolewa kwa Maximo mchezaji huyo alisema kuwa mifumo ya kiuchezaji ya Maximo ilichangia kwa kiasi kikubwa kushindwa kucheza kwa utulivu. Coutinho ni mchezaji mwenye uwezo mkubwa wa kupiga mipira iliyokufa, labda hiyo ndiyo sababu kubwa inayomfanya kuingia moja kwa moja katika kikosi cha Hans kwa kuwa soka la kisasa linahitaji mchezaji kama yeye katika timu.

 ' MTAALAMU WA MIKWAJU ILIYOKUFA'

Katika michuano ya Mapinduzi mapema Januari hii, Coutinho alifunga mabao matatu katika michezo minne, alifunga mara moja kwa mpira wa kona ya moja kwa moja, pia alifunga mara moja kwa mpira wa ' freekick'. Katika michezo saba ya ligi kuu chini ya Hans, Yanga imefanikiwa kufunga magoli tisa; magoli manne yakitokana na mipira ya Coutinho, licha ya kupiga kona mbili zilizozaa mabao katika mchezo dhidi ya Prisons Alhamis hii,

 Mbrazil huyo ndiye aliyehusika na goli pekee katika ushindi wa Yanga dhidi ya Coastal Union mwanzoni mwa mwezi huu. Katika mchezo huo uliofanyika katika uwanja wa Mkwakwani, nahodha wa Yanga SC, Nadir Haroub alifunga goli pekee akiunganisha mpira wa kona uliopigwa na Coutinho. Yanga imeshinda michezo minne kati ya saba iliyopita katika ligi kuu. Michezo mitatu wameshinda katika viwanja vigumu vya ugenini ( jamhuri, morogoro, mkwakwani, Tanga na Sokoine, Mbeya) na kote huko walitegemea zaidi mipira iliyokufa ya Coutinho.

' ANAPIGA MASHUTI HATA AKIWA KATIKA SPIDI'……

 Goli la pili ambalo Yanga walipata katika mchezo dhidi ya Prisons lilitokana na ' kiki kali' iliyopigwa na Coutinho. Hadi anatoka uwanjani mwishoni mwa mchezo watazamaji na mashabiki waliouzulia mchezo hvo walikuwa wamekoshwa na mchango wake katika timu. Aliwapiga sana chenga za mahudhi walinzi wa Prisons, huku kiwango chake cha kupiga pasi fupi na ndefu kikiambatana na uwezo wa hali ya juu katika kumiliki mpira. Ni kipaji halisi cha mwanasoka kutoka Brazil na bila shaka Yanga itaendelea kupata faida kubwa kutoka kwa Coutinho.

 0714 08 43 08



Comments