‘MANJI AMESHAMALIZA BIASHARA YA MAXIMO YANGA SC, KUNA HAJA YA KUMTAZAMA PIA…’



'MANJI AMESHAMALIZA BIASHARA YA MAXIMO YANGA SC, KUNA HAJA YA KUMTAZAMA PIA…'

Na Baraka Mbolembole, Dar es Salaam,

Yusuph Manji mwenyekiti wa Yanga SC amebariki kuvunjwa kwa benchi la ufundi la timu hiyo ambalo lilikuwa chini ya mkufunzi mkuu, Marcio Maximo na wasaidizi wake, Leonardo Leiva, Salvatory Edward na sasa timu hiyo itakuwa chini ya mwalimu, Mholanzi, Hans Van Der Pluijm ambaye ameingia mkataba wa mwaka mmoja sambamba na msaidizi wake, Charles Boniface Mkwassa ' Master'.

Maximo aliingia mkataba wa kuinoa Yanga akitokea klabu ya Associacao Atletica Francana ya ligi ya Serie A nchini Brazil. Yanga ilimpatia mkataba wa miaka miwili mwezi Juni mwaka huu, na mwalimu huyo alibeba matarajio ya wengi, sit u watu wa Yanga bali wapenzi wengi wa kandanda nchini walivutiwa na kitendo cha Yanga kumrejesha kocha huyo aliyeifubdisha timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars kwa miaka minne mfululizo.

Kati ya 29 Juni, 2006-Julai, Maximo alikuwa kocha wa Stars na huko aliweza kuisaidia timu hiyo kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani, CHAN, 2009, Ivory Coast. Baada ya kuondoka Stars, Maximo alipata kazi ya kuifunza klabu ya Esporte Clube Democrata ya nchini Brazil, alitimuliwa kazi baada ya miezi miwili kufuatia matokeo mabaya.

Alitua Yanga 28 June lakini siku ya Leo ( 19 Disemba) Yanga inathibisha kumtimua kazi. Mba 24 wa Mbinu zake za kiuchezaji zilichukuliwa kama kigezo cha yeye kumbeba katika kazi yake kwani mabingwa hao mara 24 wa kihistoria wa Tanzania Bara ni timu inayopendelea soka la mbinu na ufundi na Maximo alithibisha ubora wake wakati akiwa kocha wa Stars kwakuwa aliisaidia timu hiyo kuwa ngumu kufungika.

Akiwa amewasajili wachezaji wawili raia wa Brazil, kijana wa miaka 24 Andrey Countinho na mshambulizi aliyetajwa kuwa na uzoefu Geilson Santos Santana ' Jaja' mwenye miaka 29, Maximo aliitengeneza Yanga kwa kuwategemea zaidi wachezaji hao. Hawakumuangusha kwani , Countinho akicheza katika wingi ya kushoto alifanikiwa kufunga mabao matatu katika michezo ya maandalizi, huku Jaja akifunga mabao sita kabla ya kuanza kwa msimu ( magoli mawili akifunga dhidi ya Azam FC katika mchezo wa Ngao ya Jamii).

Mchezo wa kwanza tu wa ligi ulikuwa ni ' mzito' kwa Jaja na Coutinho , walificha na vijana Salimu Mbonde na Hassan Ramadhani wakati Yanga ilipocheza na Mtibwa Sugar na kamwe hawakuwahi kuamka na kufikia uwezo wao ambao ulionekana wakati wa michezo ya maandalizi huko Zanzibar. Maximo aliendelea kuwang'ang;ania wachezaji hao licha ya Hussein Javu, Jerry Tegete na Hamis Kizza kuonekana walio bora zaidi ya Jaja ambaye goli lake pekee kufunga katika ligi kuu lilikuwa ni dhidi ya Stand United.

Yanga imepoteza michezo miwili kati ya saba msimu huu, wala hilo halikuwa tatizo la kumfanya Maximo kupoteza kazi yake ndani ya miezi mitano, bali namna Mbrazil huyo alivyokuwa akitaka kuiendesha Yanga wengi wasingekuwa tayari kumvumilia. Ni mtu yuleyule asiyeshahurika kama ilivyokuwa wakati akiinoa Stars. Yanga ni timu yenye presha kubwa, si kwa wachezaji tu hata mwalimu unapokuwa mwalimu wa klabu hiyo ni lazima uwe tayari ' kuwatii'.

Maximo angeweza kuwa mtiifu mbele ya Manji lakini shinikizo ambalo aliliweka ili timu hiyo isishiriki michuano ya Kagame Cup katikati ya mwei Agosti lilionesha nguvu ya ushawishi ya mwalimu huyo ilivyo mbele ya uongozi. Yanga haikuwa na sababu ya kugomea michuano ile lakini kilicho wazi ilikuwa ni ' uoga' wa Maximo kuanza kukosolewa mapema na kuwa katika presha, kwa kuwa tayari timu hiyo ilikuwa na maandalizi ya mwezi mmoja na siku kadhaa lakini Maximo akuwa tayari na nafasi iliangukia kwa AZam FC ambao walifanikiwa kufika hatua ya robo fainali.

Presha ya mashabiki wa Yanga ndiyo iliyomuondoa Jaja ambaye ' bila kusemwa, semwa, aliamua mwenyewe kukaa kando' na kuomba mkataba wake uvunjwe. Maximo alitumia nafasi hiyo kumsajili kiungo Mbrazil, Emerson Oliveira na kumkata mshambulizi Kizza ambaye Yanga wenyewe wanamchukulia kama mshambulizi bora zaidi wa kigeni kuichezea timu yao katika kipindi cha muongo mmoja uliopita.

Alikuwa akiwapeleka tu viongozi wa Yanga na kuwaambia, ' nakuja na Fulani, Fulani hatukuja, na Fulani aachwe'. Tunaposema kuwa walimu wawe huru kusikilizwa na kutimiziwa matakwa yao ya kizazi si kwa maana ya uongozi ukubali hata ushauri mbaya. Utawala wa Manji unaamini katika pesa zaidi, lakini ukweli haziwezi kununua mafanikio kama zinatumika kwa mipango mibaya. Yanga chini ya Manji imekuwa ikifanya maandalizi ya gharama kubwa sana lakini hakuna jambo jipya ndani ya uwanja.

Manjhana washauri?. Kama anao basi, wanamshahuri vibaya kwa kuwa alilipa pesa nyingi wakati alipovunja mkataba wa Tom Saintifiet, pia ilikuwa hivyo kwa Ernie Brandts na sasa watalazimika kumlipa Maximo na Leiva zaidi ya Bilioni moja. Je, Yanga wana mradi gani wa kutumia pesa zote hizo kuwalipa watu ambao hawafai?. Malengo ya Manji ni kuisaidia Yanga kuwa na uwanja wake, lakini kama natumia kiasi kikubwa cha pesa kulipia fidia ya kuvunja mikataba ya makocha bila shaka naweza kusema hakuna anachoweza kufanya ikiwa anamaliza miezi sita ya mwanzo kati ya 12 aliyoomba kuongoza klabu hiyo.

Majuzi nilikwenda klabuni na kudadisi mambo mengi kuhusiana na mradi wa uwanja, ni kweli Wachina walikuwepo pale Kaunda Stadium mwezi Septemba na kupima eneo hilo ambalo litajazwa kifusi ili kupanyanyua kuu kuepuka bonde lililopo uwanjani hapo. Maximo alisimamia pia zoezi hilo lakini sasa hatahusika na chochote. Yanga inaweza kumlipa Maximo na kuendelea na maisha yao.

Wakati pia wa kuuchunguza ubora wa Manji katika utawala wa mpira vinginevyo timu hiyo inaweza kuingia katika matatizo makubwa chini ya uongozi mpya hapo mwakani. Kuna vitu haviendi sawa katika utawala wa Manji ndiyo maana kila timu anabadilisha watu wa kufanya nao kazi. Manji ameshamaliza 'biashara ya Maximo, Yanga SC, Daima mbele, nyuma mwiko'



Comments