SIMBA YAKUBALI KIEMBA KUTUA AZAM FC KWA MKOPO


SIMBA YAKUBALI KIEMBA KUTUA AZAM FC KWA MKOPO

Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
kiemba

BAADA ya mvutano wa takriban mwezi mmoja, uongozi wa Simba SC ya jijini Dar es Salaam umemruhusu kiungo wake Amri Kiemba kujiunga kwa mkopo na mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) katika kipindi hiki cha usajili wa dirisha dogo.
Azam FC, mabingwa wapya wa VPL, walipeleka ombi la kumnyakua kwa mkopo kiungo huyo mkongwe siku chache baada ya uongozi wa Simba SC kumsimamisha 'kienyeji' Kiemba mara tu baada ya timu yao kuambulia sare ya 1-1 katika mechi iliyoonekana kama imeshinda dhidi ya Tanzania Prisons kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine mjini Mbeya Oktoba 25, mwaka huu.
Mara tu baada ya mechi hiyo, uongozi wa Simba ukiongozswa na Rais wake mpya, Evans Aveva ulikutana kwa kikao kizito na wachezaji kwenye hoteli ambayo timu hiyo ilikuwa imefikia mjini Mbeya na baadaye kuamua kuwasimamisha 'kienyeji bila kuwapa barua' na kuwarejesha jijini Dar es Salaam Kiemba, kiungo mpya Shaban Kisiga na winga Haroun Chanongo kwa madai ya kuihujumu timu kwa utovu wa nidhamu na kucheza chini ya kiwango.
Hata hivyo, baadaye Kisiga alisamehewa wakati Kiemba na Chanongo wakiendelea kuwa kwenye hali ya 'moshi mweusi' huku uongozi wa Simba SC ukiitaka Azam FC kumnunua Kiemba badala ya kumchukua kwa mkopo.
Simba pia walitaka wabadilishane wachezaji na Azam FC kwa kumchukua beki Said Morad ili wamwachie Kiemba kwenda kwa matajiri hao wa Dar es Salaam.
Lakini, leo mambo yamebadilika na kutengua kauli kisha kukubali kumpeleka Kiemba Azam FC kwa mkopo.
Msemaji wa Simba SC, Hamphrey Nyasio, amesema leo kuwa uongozi umekubali kiungo huyo atue Azam FC kwa mkopo kipindi hiki cha dirisha dogo baada ya kukaa vikao kadhaa.
Nyasio amedai kuwa maamuzi hayo pia yamefikiwa baada ya uongozi kushauriana na benchi la ufundi linaloongozwa na Mzambia Patrick Phiri ambaye jana alirejea kwao kwa mapumziko ya wiki moja kabla ya kuanza maandalizi ya mechi yao ya 'Nani Mtani Jembe 2′ dhidi ya Yanga iliyopangwa kupigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini hapa Desemba 13, mwaka huu.
"Ni maamuzi ya kawaida, hasa kipindi hiki cha usajili. Uongozi haujakurupuka katika hili, maamuzi yamefanywa baada ya kupata baraka za mwalimu (Phiri)," amesema Nyasio.
Kiemba, ambaye amekuwa na wakati mgumu katika kikosi cha Simba SC akituhumiwa kucheza vizuri Taifa Stars na kucheza ovyo akiwa klabuni, aliongeza mkataba wa miaka miwili kuitumikia klabu hiyo ya Msimbazi msimu uliopita, mkataba uliomfanya awe miongoni mwa wachezaji wanaolipwa vizuri Simba SC.



Comments