Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
          BAADA ya mapumziko ya wiki mbili, Kocha wa Yanga, Marcio Maximo          anatarajiwa kurejea nchini Jumatano akiwa na Wabrazil wenzake;          msaidizi wake Leonado Neiva, viungo Andrey Coutinho na Emerson          De Oliveira Neves Rouqe anayekuja kufanya majaribio.
          Timu ya Yanga baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya          Mgambo Shooting katika mechi iliyofinyangwa na maamuzi mabovu ya          refa Ngole Mwangole kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam,          ilikwenda mapumziko ya wiki mbili kabla ya kuanza kuipashia          Simba kwa ajili ya mechi yao ya 'Nani Mtani Jembe 2′.
          Yanga iliyo nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom          Tanzania Bara (VPL), itaanza mazoezi kwenye uwanja wa shule ya          sekondari Loyola jijini Dar es Salaam Jumatano kujiandaa kwa          mechi ya 'Nani Mtani Jembe 2′ dhidi ya Simba itakayochezwa          kwenye Uwanja wa Taifa jijini Desemba 13.
          Katibu Mkuu wa Yanga, Beno Njovu amesema jijini leo kuwa Maximo          na nyota hao watatua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa          Julius Nyerere (JNIA) jijini Jumatano, tayari kuanza kwa          maandalizi ya mechi hiyo dhidi ya Simba pamoja na mechi          zinazofuata za VPL, wakiwa na mechi ngumu ya raundi ya nane          dhidi ya Azam FC Desemba 28.
          "Timu inaanza mazoezi siku ya Jumatano, kocha pamoja na nyota          wetu kutoka Brazil watawasili pia siku hiyo. 'Coach' (Maximo)          atakapowasili ndiyo ataamua kama kuna umuhimu wa kuweka kambi na          ni wapi kambi iwekwe," amesema Njovu.
          Emerson anakuja kufanya majaribio Yanga baada ya timu hiyo ya          Jangwani kuthibitisha mwishoni mwa wiki kuachana na mshambuliaji          wake Mbrazil Geilson Santos Santana 'Jaja'.
          Licha ya kufunga magoli mawili mazuri katika ushindi wa 3-1          dhidi ya Azam FC katika mechi ya Ngao ya Jamii msimu huu          iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa Septemba 14, Jaja amekuwa na          wakati mgumu kikosini Yanga baada ya kuwa butu VPL akifunga goli          moja tu katika mechi saba za mwanzo.
          Aidha, wakati mazoezi ya uwanjani yakianza Jumatano, Njovu          ameweka wazi kwamba wachezaji wao wameanza mazoezi ya gym leo          jijini Dar es Salaam chini ya kocha msaidizi Shadrack Nsajigwa          'Fuso'.
Comments
Post a Comment