Bao la dakika ya 85 lililofungwa na Wayne Rooney, lilikuwa tukio muhimu lililowapa Manchester United pointi tatu muhimu dhidi ya Arsenal.
Marouane Fellaini alichukua mpira uliokolewa na mabeki wa United, akampigia pasi ndefu Di Maria ambaye nae akamsogezea Rooney aliyekimbia na mpira na kwenda kumchambua kipa Damian Martinez aliyeingia kuchukua nafasi ya Wojciech Szczesny aliyeumia.
United iliyokuwa ugenini ilicheza soka la kawaida sana na ilikuwa vigumu kuamini kama wataambulia hata sare Emirates, lakini shuti la Antonio Valencia la dakika ya 56, lililosindikizwa wavuni na beki wa Arsenal, Kieran Gibbs, likabadilisha mwelekeo wa mchezo na hatimaye United ikaibuka na ushindi wa 2-1.
Mshambuliaji wa Arsenal Olivier Giroud ambaye ndiye kwanza anarejea uwanjani baada ya kuwa majeruhi kwa muda mrefu, akaifungia Arsenal bao la kufutia machozi dakika ya 90.
Arsenal walitawala mchezo kwa kila hali lakini tatizo kubwa likawa ni namna ya kumtungua kipa David De Gea.
United iliendelea kuzama kwenye janga la majeruhi baada ya kumpoteza mapema beki wake Luke Shaw aliyemia dakika ya 16 na nafasi yake kuchukuliwa na Ashley Young.
Kwa upande wa wenyeji, mbali na kumpoteza kipa wake, Arsenal pia iliathirika kwa kuumia kwa kiungo wake Jack Wilshere aliyeumia dakika ya 56 na nafasi yake ikazibwa na Santi Cazorla.
Kwa ushindi huo, United imesogea hadi nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya England ikitanguliwa na Southampton, Manchester City na vinara Chelsea.
Arsenal: Szczesny, Chambers, Mertesacker, Monreal, Gibbs, Arteta, Ramsey, Sanchez, Wilshere, Oxlade-Chamberlain, Welbeck.
Man Utd: De Gea, Smalling, McNair, Blackett, Shaw, Carrick, Valencia, Fellaini, Rooney, Di Maria, van Persie.
Comments
Post a Comment