Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
          MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL),          Azam FC baada ya mapumziko ya wiki mbili kesho wataanza mazoezi          kujiweka fiti kabla ya kuwavaa Yanga katika mechi yao ya raundi          ya nane ya ligi hiyo msimu huu.
          Meneja wa timu ya Azam, Jemedari Said amesema jijini Dar es          Salaam leo kuwa kikosi chao kitaanza mazoezi mepesi kesho          Jumatatu bila mshambuliaji wake Piere Saint Preux ambaye          amerejea kwao Haiti na kiungo Michael Bolou ambaye pia amerejea          kwao Ivory Coast.
          "Kocha msaidizi George Simbe atawasili kesho, wachezaji wanaanza          kukusanyika kesho na tutaanza mazoezi kesho pia. Tutaanza kwa          mazoezi mepesi maana wachezaji walikuwa mapumzikoni. Lazima          twende mdogo mdogo," Jemedari amesema.
          "Baada ya kuwasili kwa kocha msaidizi, itatolewa ratiba nzima          itatolewa ya mpaka Desemba 28 tutakapocheza dhidi ya Yanga."
          Amesema beki wao mpya Serge Wawa atawasili nchini Desemba Mosi          na kwamba wachezaji wao walioko kwenye kambi ya Zanzibar Heroes          kwa ajili ya michuano inayoonekana kubuma ya Kombe la Chaleni,          wataungana na wenzao kesho kwa sababu tayari uongozi wa Azam FC          umewasiliana na Chama cha Soka Zanzibar (ZFA).
          Azam itakayoiwakilisha Tanzania katika michuano ya Klabu Bingwa          Afrika mwakani, iko nafasi ya pili katika msimamo wa VPL ikiwa          na pointi 13 sawa na Yanga walioko nafasi ya tatu, Nafasi ya          kwanza inakaliwa na mabingwa wa Tanzania Bara 1999 na 2000,          Mtibwa Sugar.
Comments
Post a Comment