Tanzania Prisons vs Simba SC, Ukubwa wa Simba upo kwa mashabiki tu…


Tanzania Prisons vs Simba SC, Ukubwa wa Simba upo kwa mashabiki tu…

Na Baraka Mbolembole,

Tanzania Prisons ni moja ya timu ngumu zikiwa katika uwanja wa nyumbani, timu hiyo huwa ngumu zaidi inapocheza na Simba katika uwanja wa Sokoine, Mbeya. Katika michezo miwili ya msimu uliopita, Simba ilishinda katika uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa mabao 3-1. Katika mchezo wa marejeano timu hizo hazikufungana katika uwanja wa Sokoine.

" Kuna majeruhi kadhaa katika kikosi changu lakini hakuna kitakachoharibika katika mipango yangu" anasema, David Mwamaja kocha wa Prisons ambaye ataendelea kukosa huduma ya mshambulizi wake hatari, Peter Michael ambaye alifunga mabao 12 msimu uliopita.

SONY DSC

"Simba ni Simba tu, ni timu kubwa nchini hilo tunalitambua, lakini usisahau kuwa Prisons ni timu kubwa pia" anaongeza kusema, Mwalimu huyo ' mnene zaidi' katika ligi kuu ya Tanzania Bara ambayo inaingia katika mzunguko wa tano wikendi hii. " Prisons ni timu kubwa, wakati fulani mambo hayakuwa mazuri na timu ikashuka daraja. Ukubwa wa Simba upo kutokana na wingi wa mashabiki wa timu hiyo ambao ni wengi tofauti na wale wa Prisons".

Simba ni mabingwa mara 19 wa ligi kuu Bara, wakati, Prisons walipoteza nafasi ya kutwaa ubingwa huo mara kadhaa. Tanzania Prisons ni mabingwa wa zamani wa Tanzania, 1998 walishindwa kutwaa ubingwa wa Bara, 2002 licha ya kuhitaji sare tu katika mchezo wa mwisho dhidi ya Yanga katika uwanja wa Sokoine.

Msimu wa 2007/08 timu hiyo ya Mbeya iliongoza ligi kwa tofauti ya pointi 11 hadi mzunguko wa kwanza uliopomalizika, lakini walipigwa kumbo kwa mara nyingine na Yanga ambao walifanikiwa kuchukua taji huku Prisons wakimaliza katika nafasi ya pili. Mambo yalikuwa magumu kwa timu hiyo msimu wa 2008/09 msimu ambao timu hiyo ilishuka daraja na kucheza ligi ya chini kwa misimu miwili kabla ya kurejea tena katika ligi kuu msimu wa 2012/13.



Comments