Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
ISMAIL Aden Rage, aliyekuwa mwenyekiti wa Simba, ameuomba          uongozi mpya wa klabu hiyo kutomtimua kocha Patrick Phiri          kutokana na matokeo mabovu ya timu yao kwa kuwa Mzambia huyo          ameikuta timu ikiwa na hali mbaya.
          Uongozi mpya wa Simba chini ya Rais Evans Aveva umemtaka Phiri          ashinde mechi mbili zijazo dhidi ya vinara wa msimamo Mtibwa          Sugar na Ruvu Shooting, vinginevyo kibarua chake katika klabu          hiyo ya Msimbazi kitaota nyasi.
          Akizungumza katika kipindi cha 'Spoti Leo' cha Radio One usiku          wa kuamkia leo, Rage amesema Phiri amerudi Simba katika kipindi          kigumu, hivyo anapaswa kupewa nafasi zaidi ya kukisuka kikosi          cha timu hiyo.
          "Phiri amekuja muda wakati mbaya Simba, Tuna matatizo ya          'defence' (ulinzi) tangu kuondoka kwa (Donald) Mosoti. Sijui kwa          nini beki huyo aliondolewa Simba," amesema Rage.
          "Kama ningelikuwa bado kiongozi wa Simba, ningeangalia mchezaji          mwingine wa kumwacha badala ya Mosoti, kwanza jina lake tu,          anatisha yule kijana," ameongeza Rage huku akikosoa vikali          vitendo vinavyoashiria ushirikina vilivyotawala Ligi Kuu ya          Vodacom Tanzania Bara (VPL) msimu huu.
          
          Amesema kuwa watu wanaoamini ushirikina, hawana imani ya Mungu          huku akipinga pia kusimamishwa kwa wachezaji watatu wa Simba;          viungo Amri Kiemba na Shabani Kisiga pamoja na winga Haroun          Chanongo.
          "Ninawaheshimu viongozi wapya wa Simba kwa sababu ni viongozi          wetu. Ninaamini mazungumzo yao na wachezaji waliosimamisha          yatakuwa mazuri na watawarejesha kikosini kwa sababu tatizo la          Simba ni kuondoka kwa Mosoti," amesema.
          "Kama hutaki sare na kufungwa, usiingie kwenye mashindano. Sisi          tunachotakiwa ni kujifunza kwa nchi zilizoendelea kisoka,          kuandaa timu kuanzia timu za vijana. Inashangaza kuona          tunawekeza zaidi katika imani za kishirikina," amesema zaidi          Mbunge huyo wa Tabora Mjini (CCM).
          Simba iliyokamata nafasi ya 10 katika msimamo wa VPL baada ya          kuambulia sare katika mechi tano zote za mwanzo, Jumamosi          itakuwa na mtihani mgumu mbele ya kikosi cha kocha Mecky Mexime          cha Mtibwa Sugar ambacho hakijapoteza mechi hata moja tangu          kuanza kwa msimu Septemba 20 kikiongoza ligi kwa kushinda mechi          nne na kutoka suluhu mara moja dhidi ya Pilisio Morogoro.
          Simba haijapata ushindi kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro          dhidi ya mabingwa hao mara mbili mfululizo wa Tanzania Bara 1999          na katika mwaka wa mabadiliko ya karne tangu iliposhinda 2-1          msimu wa 2011/12. Timu hiyo ya Msimbazi ilifungwa 2-0 na          wakatamiwa hao wa Manungu, Turiani msimu wa 2012/13 kabla kutoka          sare ya bao moja msimu uliopita.
Comments
Post a Comment