KUNDI la G Five Modern Taarab, Alhamisi hii limeingia studio za Sound Crafters jijini Dar es Salaam kurekodi wimbo mpya utakaoimbwa na Abdul Misambano.
Wimbo huo unakwenda kwa jina la "Si mie ni moyo" utunzi wake Misambano mwenyewe.
Ndani ya wimbo huo utakutana na kinanda kitamu cha Omar Kisila huku gitaa zito la bass likikung'utwa na Mussa Mipango.
Kweye gitaa linaloongoza (solo) kuna mkono wa Jumanne Ulaya.
Baada ya kutamba sana na wimbo wa "Asu" zaidi ya miaka 15 iliyopita, ujio mpya wa Misambano umekuwa ukisubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa taarab.
Hiyo haimaanishi kuwa Misambano hajatoa nyimbo nyingine baada ya Asu, lakini ukweli ni kwamba hakuna wimbo wake uliopiku makali ya Asu.
Je "Si mie ni moyo" utaipiku Asu? Ni suala la kusubiri.





Comments
Post a Comment