Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
          MECKY Mexime, kocha mkuu wa Mtibwa Sugar, amesema hana muda wa          kufikiri kuhusu sharti la kuifunga timu yake lililotolewa na          uongozi wa Simba kwa benchi la ufundi timu hiyo ya Msimbazi          badala yake atawajibu uwanjani wakati timu hizo zitakapopambana          katika mechi ya raundi ya sita ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania          Bara (VPL) kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro Jumamosi.
          Akizungumza na mtandao huu akiwa kambini Manungu, Turiani jana          mchana, Mexime alisema Simba ni wataalam wa kuongea lakini          akawataka kuelewa kwamba kikosi chake kimejipanga kufanya kweli          msimu huu.
          "Kuna maneno mengi yanasemwa kuhusu mechi yetu dhidi ya Simba.          Mara lazima makocha wao washinde mechi yetu, vinginevyo          watafukuzwa, hayo ni maneno tu. Kazi itakuwapo uwanjani          Jumamosi," amesema Mexime.
          Nahodha huyo wa zamani wa Mtibwa Sugar na Taifa Stars amesema          kikosi chake kiko salama na kinaendelea kujifua kambini Manungu          km 100 kutoka mji wa Morogoro na kitaingia mjini humo Jumamosi          tayari kuikabili Simba.
          " Tunamshukuru Mungu hatuna mchezaji anayeumwa, tutajibu tambi          za Simba uwanjani kwa sababu msimu huu tumepania," ameongeza          kocha huyo aliyeweka wazi kwamba msimu huu Mtibwa itamaliza          katika moja ya nafasi mbili za juu.
          Mtibwa Sugar inayoongoza msimamo wa ligi ikiwa na pointi 13,          tatu mbele ya Azam na Yanga zilizopo nafasi za pili na tatu,          haiojafungwa na Simba kwenye Uwanja wa Jamhuri tangu msimu wa          2011/12 ilipopoteza 2-1 kabla ya kushinda 2-0 msimu wa 2012/13          na kutoka sare ya bao moja msimu uliopita.
          Usajili wa mshambuliaji Ame Ally Shomary kutoka Chuoni FC ya          Ligi Kuu ya Zanzibar, kumeiimarisha zaidi safu ya ushambuliaji          ya Mexime ikifunga magoli nane huku safu ya ulinzi ikiruhusu          goli moja tu, tofauti na Simba waliofunga magoli matano na          kufungwa matano pia.
          Safu ya ulinzi ya Simba iliyopwaya mno baada ya kutemwa kwa beki          Mkenya Donald Mosoti itakuwa na wakati mgumu mbele ya          washambuliaji Ame, Musa Mgosi na Vicent Barnabas ambaye mara          nyingi amekuwa akitokea benchini na kufanya 'vitu vya maana'.
          Mtibwa imepanga kushinda mechi 10 kati ya 13 mzunguko wa kwanza          wa VPL msimu huu.
Comments
Post a Comment