Na Bertha Lumala, Dar es Salaam
          Kocha mkuu wa Simba, Mzambia Patrick Phiri amesema kuvunjwa kwa          mkataba wake hakutakuwa na manufaa yoyote kwa klabu hiyo ya          Msimbazi iliyopoteza ghafla matumaini ya kutwaa ubingwa wa Ligi          Kuu Tanzania Bara.
          Simba iliyoko nafasi ya 10 katika msimamo wa ligi hiyo,          imeambulia sare tano mfululizo katika mechi tano zilizopita hali          iliyopelekea uongozi kumtaka kocha huyo ashinde mechi mbili          zijazo, vinginevyo atatimuliwa.
          Akiwa mjini Iringa ambako timu yake leo jioni inacheza mechi ya          kirafijki dhidi ya Lipuli kujiandaa kwa mechi ya raundi ya tano          dhidi ya Mtibwa Sugar Jumamosi, Phiri amesema ajira yake si          suala muhimu Simba bali wanapaswa kuumiza vichwa kufikiri namna          ya kuisaidia timu hiyo kongwe nchini.
          Kocha huyo alikiri kupewa taarifa hiyo na uongozi wa juu wa          Simba uliokuwa mjini Mbeya mwishoni mwa wiki chini ya Rais wa          klabu hiyo, Evans Aveva, ambao pia uliwasimamisha na kuwataka          kurejea Dar es Salaam kwa mahojiano zaidi viungo Amri Kiemba na          Shaban Kisiga pamoja na winga Haroun Chanongo muda mfupi baada          ya timu yao kutoka sare ya 1-1 na wenye Tanzania Prisons kwenye          Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine mjini humo Jumamosi.
          "Ni kweli utawala umenipa mechi mbili kuhakikisha timu          inashinda, kinyume chake wamesema watavunja mktaba wangu. Lakini          ajira yangu Simba si suala muhimu kwa sasa kulijadili. Kilicho          muhimu kwetu kwa sasa ni kuangalia matatizo yanayoikabili timu          na kuyatafutia dawa," amesema Phiri.
          "Mimi nina muda mfupi, sidhani kama ajira yangu ni tatizo          Simba," ameongeza kocha huyo mwenye historia ya kuipa ubingwa wa          Tanzania Bara timu hiyo bila kupoteza hata mechi moja.
          Simba anainoa Simba kwa awamu ya tatu baada ya kuifundisha pia          2005 na 2010. Ni kocha wa 18 kuifundisha timu hiyo ndani ya          miaka 16 tangu 1998
Comments
Post a Comment