SANCHEZ AIPA JEURI ARSENAL …WENGER ASEMA HANA MPANGO WA KUNUNUA MSHAMBULIAJI …akanusha kuwataka Nikola Zigic na Danny Welbeck
ARSENEL Wenger hana mpango wa kusajili mbadala wa mshambuliaji Olivier Giroud – haswa baada ya lexis Sanchez aliyefunga bao la ushindi dhidi ya Besiktas kuthibitsha kuwa anakidhi vigezo vyote vya kuongoza safu ya ushambuliaji ya Arsenal.
Giroud ameumia enka na anaweza akawa nje ya dimba hadi mwaka ujao na hivyo kupelekea Arsenal kuhusishwa na tetesi za usajili wa washambuliaji wengi kwaajili ya kuziba pengo la mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 27.
Lakini Sanchez aliyesajiliwa kiangazi hiki kutokea Barcelona, jana usiku alifunga bao lililoipeleka Arsenal hatua za makundi ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya ikiwa ni mara ya 17 mfululizo kwa timu hiyo.
Licha ya Arsenal kuwa pungufu kwa mrefu baada ya beki Mathieu Debuchy kulimwa kadi nyekundu, bao la dakika 45 la Sanchez likatosha kuivusha Arsenal kufuatia sare ya 0-0 ya mchezo wao wa kwanza.
Baada ya Sanchez kuiwezesha Arsenal kuvuka kitanzi hicho, Wenger akamtupia sifa kibao na kusema: "Nilimnunua aje kucheza kama mshambuliaji".
Wenger akakanusha uvumi wa kumtaka Nikola Zigic au Danny Welbeck na kusisitiza kamwe hataingia sokoni na kufanya manunuzi ya hamaki eti kisa Giroud ameumia.
Alipoulizwa kuhusu tetesi za kutaka kumsajili mshambuliaji wa Serbia mwenye urefu wa futi 7 na inchi 6, Wenger akajibu: Nani? Zigic? Hapana.
"Utaniuliza kuhusu nani nitamnunua. Nitakupa jibu – kwa sasa jibu ni Hapana," alisema.
"Kama unataka kumfanya kila mtu awe na furaha, basi utanunua wachezaji wote hao lakini kilicho muhimu ni kiwango uwanjani. Ukitazama wachezaji walioko benchi na wale majeruhi utagundua kuwa tuna wachezaji wa kutosha. Huwezi kununua mchezaji kila unapokuwa na majeruhi."
Comments
Post a Comment