Marijani Rajabu         Marijani Rajabu          kwa vyovyote ni mmoja wa wanamuziki ambao wametoa mchango mkubwa          katika ulimwengu huu wa muziki. Japo ni miaka mingi toka mauti          yake yalipomfika, bado nyimbo zake zinapigwa na wanamuziki          mbalimbali majukwaani na hata kurudiwa kurekodiwa tena. Marijani          alizaliwa maeneo ya Kariakoo mwaka 1954. Mama yake alikuwa mama          wa nyumbani wakati baba yake alikuwa na shughuli za uchapishaji.          Maisha yake ya utoto yalikuwa ya kawaida ila alikuwa kipenda          sana uimbaji wa Tabu Ley na mwimbaji mmoja wa Guinea Sorry          Kandia. Alilelewa vizuri kwa misingi ya dini ya Kiislam kwa          hivyo alihudhuria mafunzo ya dini utotoni kama inavyotakiwa.          Akiwa na umri wa miaka 18 hivi, alijiunga na STC Jazz, ikiwa          chini ya mpiga gitaa maarufu wakati huo Raphael Sabuni, kabla ya          hapo bendi hii ilikuwa unajulikana kama The Jets. Katika bendi          hii Marijani aliweza kutoka nje ya Tanzania kwa mara ya kwanza          ambapo alikwenda Nairobi na kurekodi nyimbo zilizotoka katika          label ya Phillips. Mwaka 1972 Marijani alihamia bendi ya Safari          Trippers. Hapa ndipo ubora wake ulifunguka haswa na kuweza          kuinyanyua Safari Trippers kuwa moja ya bendi maarufu za wakati          huo. Waliweza kutoa vibao vilivyopendwa mfululizo na kuweza          kuzunguka nchi nzima. Vibao kama Rosa nenda shule,          Georgina,Mkuki moyoni, viliweza kuuza zaidi ya nakala 10000 za          santuri na hivyo kuwezesha bendi kuwa na vyombo vyake vizuri.          Bendi wakati huo ikiwa na wanahisa wanne, ambao kwa bahati mbaya          wakati bendi ndio iko juu, wakakosa kuelewana na ukawa ndio          mwisho wa bendi hiyo. Miezi michache baadae Marijani na wenzie          waliibukia Dar International. Pia huku kulikuwa na wanamuziki          wazuri na haraka bendi ilipata umaarufu wa hali ya juu kwa vibao          vyake kama Zuena na Mwanameka. kutokana na hali wakati huo bendi          ilirekodi vibao hivi RTD na kuambulia sh 2500/- tu.          Kilichosikitisha zaidi ni kuwa nyimbo zao tisa ziliuzwa kwa          kampuni ya Polygram bila ridhaa yao. Kati ya mwaka 1979 na 1986          bendi ilipiga karibu kila wilaya nchi hii na kufurahisha sana          watu na mtindo wao wa Super Bomboka. Uchakavu wa vyombo hatimae          mwaka huo 1986, ukamaliza mbio za bendi hii. Kwa miezi michache          Marijani akashiriki katika lile kundi kubwa la wanamuziki 57          waliotengeneza Tanzania All Stars, kundi hili lilirekodi vibao          vinne ambavyo si rahisi kwa bendi zilizopo sasa kufikia ubora          wake kimuziki. Marijani alipitia Mwenge Jazz kw muda mfupi, na          kukaa kama mwaka mmoja Kurugenzi Jazz ya Arusha, kisha akajaribu          kuanzisha kundi lake la Africulture na mtindo wa Mahepe lakini          kwa ukosefu wa vyombo mambo hayakuwa mazuri. Kufiki1992 hali ya          Marijani ilikuwa ngumu akiishi kwa kuuza kanda zake ili aweze          kuishi.Pamoja na nyimbo nyingi, za kuimbia Chama tawala na          serikali, na hata tungo yake Mwanameka kutumiwa katika mtihani          wa kidato cha Nne. Rajabu Marijani hajawahi kukumbukwa rasmi          kama mmoja wa wasanii bora Afrika ya Mashariki 
                
 
Comments
Post a Comment