Castle Lager Perfect Six ngazi ya mikoa yaanza



Castle Lager Perfect Six ngazi ya mikoa yaanza
Mashindano ya Castle Lager Perfect Six ngazi ya mikoa yameanza kutimua vumbi wikendi hii ambapo jumla ya timu 48 zimeshuka dimbani katika mikoa ya Dar na Morogoro zikiwania nafasi ya kufuzu kushiriki ngazi ya kanda na hatimaye fainali za kitaifa.

Meneja wa Bia ya Castle Lager, Kabula Nshimo alisema kuwa mechi zilizochezwa wiki iliyopita zimeonyesha jinsi gani Watanzania wana mwamko na shauku kubwa ya kushiriki mashindano kutokana na watu kujitokeza kwa wingi maeneo mbalimbali ambapo yalifanyika mashindano hayo ya kwanza.

Mechi zilizochezwa wikendi hii ilikuwa ni awamu ya kwanza ya mashindano hayo ambapo timu zitakazofuzu hatua hiyo ya mikoa zitachuana katika ngazi ya kanda na hatimaye taifa. Washindi wa fainali za taifa watajipatia fursa ya kipekee kwenda kutembelea jiji la Barcelona huko Hispania na kuiona timu ya Barcelona ikicheza na pia wataweza kujionea mambo mbalimbali ya kihistoria katika uwanja wa Camp Nou.

Baadhi ya maeneo na timu zilizoshiriki ni Ilala ambapo timu zilizoshiriki ni Nato FC, Gaddafi FC, Barafu Veterani, Pata Habari, Dira ya Mtanzania, Hazard Team, Mburahati Veterans na Baracuda FC ambapo mechi hizo zilipigwa kwenye uwanja wa Rova Ashanti na Baracudda FC waliibuka washindi. Temeke ni Lumo FC, Sunset FC, Flamingo FC, Yombo Classic, Wazee wa Povu FC, Shelly FC, Mwisho wa Lami FC, na Oilcom FC ambapo mechi hizo zilipigwa kwenye uwanja wa Mwembeyanga na Gaddafi kuibuka washindi. Kwa mechi iliyochezwa uwanja wa Mwinjuma Kinondoni timu ya AUCT iliibuka washindi. Fainali za kanda ya Dar es salaam zitachezwa Juni 8 kwenye viwanja vya TCC Chang'ombe ambapo timu zilizofuzu Temeke, Ilala na Kinondoni zitachuana kupata washindi watakaoshiriki fainali za taifa.

Na huko Morogoro, timu za soka za Mzinga FC na Ndezi FC zimefanikiwa kutinga hatua ya fainali za kanda ya mashariki baada ya kufanya vizuri mashindano hayo yaliyofanyika uwanja wa Shule ya Msingi Kiwanja cha Ndege Manispaa ya Morogoro.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mara baada ya kumalizika kwa michezo iliyoshirikisha timu nane mjini hapa, Mwamuzi wa mchezo huo Elly Sasii alisema kuwa ni timu za Mzinga na Ndezi ndizo zilizofanikiwa kutinga hatua ya fainali za kanda ya mashariki ikisubiri washindi wenzao wa mkoa wa Dodoma.

Sasii alisema kuwa Mzinga na Ndezi zitacheza ligi ndogo ya mashindano hayo Juni 7 mwaka huu Manispaa ya Morogoro na washindi wa Dodoma ili kupata timu moja itayowakilisha kanda ya mashariki katika mashindano ya taifa yatayofanyika baadaye jijini Dar es Saalaam.

 "Haya mashindano hapa nchini ni mapya na lengo lake ni kupata timu moja itayoenda Hispania kushuhudia michezo ya Barcelona."alisema Sasii.

Sasii alifafanua kuwa washindi hayo walifanikiwa kushinda timu nyingine katika hatua ya mtoano, robo fainali ikihusisha timu za Misufini A na B, Nyumbani Park A na B, Airport Rangers na Mtazamo zote za Manispaa ya Morogoro.

Kanda zitakachuana ni pamoja na kanda ya mashariki, Kaskazi, kanda ya Ziwa na kanda za nyanda za juu kusini ambapo baadhi ya kanda michuano hiyo tayari zimeanza rasmi mei 24 mwaka.
 Mchezaji wa timu ya Baracuda, Jamhuri Kihwelo akifunga goli dhidi ya Nato ya Ukonga kwenye mechi ya nusu fainali iliyofanyika kwenye uwanja Rova Ashanti Dar es Salaam wiki iliyopita kwenye mashindano ya 'Castle Perfect Six' ngazi ya mikoa ambapo washindi watapata fursa ya kwenda kuiona timu ya Barcelona, Mashindano hayo yamedhaminwa na bia ya Castle Lager. Nato ilishinda kwa 5-1.
Meneja Mradi wa Bia ya Castle Lager, Willhard Malimbo kulia akiwakabidhi zawadi wachezaji wa Timu ya Gaddafi walioibuka washindi wa kwanza katika bonanza la Castle Perfect (6) lililofanyika kwenye Viwanja vya Mwembe Yanga Dar es Salaam wiki iliyopita.



Comments