SIMBA: BADO TUNA NAFASI YA KUTWAA UBINGWA VPL


SIMBA: BADO TUNA NAFASI YA KUTWAA UBINGWA VPL

Hajji Manara, Msemaji wa SimbaNa Bertha Lumala, Dar es Salaam
Timu ya Simba imesema bado ipo katika mbio za kuwania ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) kwa msimu huu kwa vile bado ligi haijamalizika na bingwa bado hajafahamika mpaka sasa.

Msemaji wa Simba SC, Hajji Manara, ameuambia mtandao huu kuwa timu yao bado ina nafasi ya kunyakua taji VPL kwa msimu huu endapo Yanga SC na Azam FC watazubaa na wao kufanya kweli katika michezo yao yote iliyobaki.

"Kimahesabu watu wanaweza wakaona Simba haina nafasi ya kuwa bingwa wa ligi kwa msimu huu, lakini kwa watu tunaoamini katika soka nafasi bado ipo na hatujakata tamaa. Kuna timu hapa zitakutana zenyewe kwa zenyewe kwa hiyo lolote linaweza kutokea," amesema Manara.

Manara amesema mbio za ubingwa wa ligi ni kama mbio za Marathon, atakaegusa kamba ndiye mshindi.

"Hatujakata tamaa kwa sababu hakuna aliyegusa kamba ya mwisho," amesema zaidi mtoto huyo wa mchezaji wa zamani wa Yanga SC, Sunday Manara.

Simba SC iko nafasi ya tatu katika msimamo wa VPL ikiwa na pointi 32, nane nyuma ya vinara Yanga SC.



Comments